Bei ya kondomu sasa yapanda na kufika Sh600
KWA zaidi ya miongo miwili, kondomu zilizokuwa zikipatikana katika baa, vyuo vikuu na hospitali nchini Kenya ziligharimiwa kwa kiasi kikubwa na serikali ya Amerika.
Hata hivyo, hali imebadilika ghafla baada ya ufadhili huo kusitishwa, na sasa nchi inakabiliwa na uhaba mkubwa wa kondomu.
Mnamo Januari 2025, Rais Donald Trump alitia saini agizo la kusimamisha misaada ya nje, hatua iliyosababisha shirika la USAID kusitisha ununuzi na usambazaji wa kondomu nchini Kenya.
Hali hii imeathiri pakubwa wanawake, vijana na wafanyakazi wa ngono ambao hutegemea bidhaa hizi kwa kinga dhidi ya maambukizi.
Bajeti ya mwaka 2027 ya sekta ya afya ya Amerika imeweka wazi msimamo huo, ikipendekeza kupunguza matumizi ya afya ya kimataifa kwa kiasi kikubwa na kusisitiza kuwa nchi hiyo haitagharamia tena kondomu au mpango wa uzazi nchini Kenya.
Uamuzi huu umeacha pengo kubwa katika juhudi za kudhibiti maambukizi ya magonjwa ya zinaa.
Kwa sasa, Kenya inahitaji takriban kondomu 400 milioni kila mwaka, lakini serikali inaweza kusambaza karibu 200 milioni pekee.
Hii inaacha pengo kubwa ambalo hapo awali lilijazwa na wafadhili wakiongozwa na USAID.
Gharama ya mpango wa kondomu ni zaidi ya Sh1.1 bilioni kila mwaka, huku upungufu ukiwa mkubwa sana.
Athari zake zinaanza kuonekana wazi miongoni mwa wananchi.
Bei ya kondomu imepanda kwa kasi, kutoka takriban Sh150 hadi kufikia Sh600 kwa pakiti.
Hali hii imefanya wengi, hasa vijana na watu wa kipato cha chini, kushindwa kuzipata kwa urahisi.
Takwimu za afya pia zinaonyesha ongezeko la magonjwa ya zinaa kama kaswende, kisonono na klamidia.
Shirika la AIDS Healthcare Foundation (AHF) limeripoti mamia ya visa vipya katika muda mfupi, hali inayoongeza hofu ya kuongezeka kwa maambukizi ya HIV/AIDS iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa.
Wataalamu wa afya wanasisitiza kuwa kondomu bado ni njia rahisi, nafuu na yenye ufanisi katika kuzuia maambukizi ya magonjwa ya zinaa.
Wanatoa wito kwa serikali na wadau wengine kuongeza uwekezaji ili kuhakikisha bidhaa hizi zinapatikana kwa wingi na kwa bei nafuu.
Hatua ya Amerika kujiondoa katika ufadhili imeiacha Kenya katika changamoto kubwa, na sasa jukumu limebaki kwa serikali na washirika wake kuhakikisha pengo hilo linazibwa ili kulinda afya ya wananchi.