Habari

Benki ya Equity yaripoti kuvuna faida kemkem ikielezea kuimarika sekta ya mikopo na akiba

Na BENSON MATHEKA August 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

EQUITY Group Holdings imeripoti ongezeko la asilimia 32 la faida baada ya ushuru katika miezi sita ya kwanza ya mwaka huu, ikiashiria kuimarika kwa biashara yake nchini Kenya na katika matawi yake ya kikanda.

Benki hiyo ilisema jana faida baada ya ushuru ilipanda hadi Sh45.5 bilioni kutoka Sh34.6 bilioni katika kipindi kama hicho mwaka jana.

Faida kabla ya ushuru iliongezeka kwa asilimia 39 hadi Sh57.8 bilioni kutoka Sh41.5 bilioni.

Ukuaji huo ulitokana na ongezeko la mapato yasiyotokana na riba na mchango mkubwa wa matawi yake katika nchi nyingine za Afrika.

Pesa zilizowekwa na wateja ziliongezeka kwa asilimia 24, huku mikopo ikikua kwa asilimia nane.

Benki hiyo pia ilirekodi ongezeko la asilimia 11 la mikopo kwa robo moja. Matawi ya kikanda pia yalifanya vizuri, yakiongozwa na Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), ambapo faida baada ya ushuru iliongezeka kwa asilimia 82 na 30 mtawalia.

Kwa jumla, mikopo ya kundi hilo iliongezeka kwa asilimia 19 hadi Sh981 bilioni kutoka Sh825 bilioni.

Wakati huo huo, mapato yasiyotokana na riba yaliongezeka kwa asilimia 36 hadi Sh55.6 bilioni, yakichangia asilimia 44.5 ya mapato yote ya kundi hilo, kutoka asilimia 40.8 mwaka jana.

Equity Insurance Group pia ilirekodi ongezeko la asilimia 24.

Ubora wa mikopo uliimarika huku mikopo isiyolipwa ukishuka hadi asilimia 9.5 kutoka asilimia 13.7, huku kiwango cha kufidia mikopo hiyo kikiongezeka hadi asilimia 70 kutoka asilimia 68.

Gharama ikilinganishwa na mapato pia ilishuka hadi asilimia 48.6 kutoka asilimia 51.7, ikiashiria kuimarika kwa ufanisi wa biashara.