Habari za Kitaifa

Wanafunzi wengi wa Gredi 9 hawawezi kusoma ipasavyo -Ripoti

Na DAVID MUCHUNGUH, MERCY SIMIYU August 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAKRIBAN thuluthi moja ya wanafunzi wanaojiunga na Sekondari Pevu kutoka Sekondari Msingi hawana ujuzi muhimu wa kusoma, kuandika na kuhesabu, ripoti mpya imefichua.

Ripoti hiyo iliyotolewa na Usawa Agenda, shirika linalofanya utafiti kuhusu elimu ya msingi, pia imeonyesha kuwa wanafunzi katika shule za umma za maeneo ya mashambani ndio walioathirika zaidi.

Utafiti huo uliofanywa katika kaunti zote 47 ulihusisha familia 41,156, shule 1,527 na wanafunzi 49,835. Pia ulihusisha jamii za wakimbizi katika kambi za Dadaab, Kakuma na Kalobeyei.

Ripoti hiyo inasema asilimia 29 ya wanafunzi wa Gredi 9 hawana ujuzi wa msingi wa kusoma na kuhesabu.

Mwanafunzi mmoja kati ya watano wa Gredi 9 hawezi kusoma hadithi ya Kiingereza ya kiwango cha Gredi 3.

Hali hiyo pia inawakumba wanafunzi watatu kati ya 10 wa Gredi 7.

Hata hivyo, pengo hilo huanza mapema zaidi. Asilimia 41 ya wanafunzi wa Gredi 7 hawana ujuzi wa msingi wa kusoma na kuhesabu.

Ripoti hiyo ilisema shule za umma hufanya vibaya kuliko shule za kibinafsi katika kusoma na kuhesabu.

“Ushahidi unaonyesha kuwa sera za serikali zimefanikiwa kuwadumisha wanafunzi madarasani, lakini bado hazijafanikiwa kuhakikisha wanajifunza au shule wanazojiunga nazo zina vifaa sawa vya kusoma,” ripoti hiyo ilisema.

Ripoti hiyo ilibaini pia upungufu mkubwa wa vifaa shuleni.

Ni asilimia 27.5 pekee ya shule za Sekondari Msingi zilizo na maabara za sayansi zinazofanya kazi, huku asilimia 27 zikiwa na maktaba.

Ni asilimia 34.3 pekee zilizo na vifaa vya kutosha vya kusoma na asilimia 46.3 zilikuwa na kompyuta za wanafunzi.

Tofauti za kikanda ni kubwa. Nairobi ina maabara zinazofanya kazi katika asilimia 98.7 ya shule za Sekondari Msingi, ikilinganishwa na asilimia 15.4 Kaskazini Mashariki na asilimia 13.8 Magharibi.

Mkurugenzi wa Idara ya Sekondari Msingi katika Wizara ya Elimu Hellen Avisa, alisema changamoto ya ujuzi wa msingi inapaswa kushughulikiwa mapema.

Alisema ushahidi uliowasilishwa unapaswa kuchochea hatua katika ngazi ya kitaifa, kaunti na shule.

Ripoti hiyo inapendekeza wanafunzi wa Gredi 7 hadi 9 wapewe masomo maalum ya kurekebisha mapengo ya kusoma na kuhesabu.

Pia inataka serikali kuongeza uwekezaji katika maabara, maktaba, vifaa vya kusoma na kuhakikisha fedha za shule zinatolewa kwa wakati.

Ripoti hiyo ilisema ni asilimia 52.3 pekee ya shule za Sekondari Msingi zinazopokea fedha kwa wakati.