Habari

Bi Nderitu ajitetea vikali uhalali wa uteuzi wake kama Kamishna mteule wa IEBC

Na CHARLES WASONGA June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MSAJILI wa Vyama vya Kisiasa nchini Anne Nderitu ametetea uteuzi wake kama Kamishna mteule wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) anapoendelea kuhusu katika afisi hiyo.

Bi Nderitu Jumamosi Mei 31, 2025 aliwaambia wanachama wa Kamati ya Bunge kuhusu Haki na Masuala ya Kikatiba (JLAC) kwamba hatua uteuzi wake na Rais William Ruto ni halali kwamba bunge halijamwidhinisha rasmi.

“Huu ni mchakato. Sijateuliwa rasmi. Sheria inatoa nafasi kwa mtu kujiuzulu wadhifa anaoshikilia hata dakika chache kabla ya kuteuliwa rasmi katika wadhifa mwingine,” Bi Nderitu akasema alipofika mbele ya kamati hiyo katika majengo ya bunge kupigwa msasa kubaini ufaafu wake kwa cheo cha Kamishna wa IEBC.

Ili kuthibitisha utetezi wake, Bi Nderitu aliwasilisha nakala ya uamuzi uliotolewa na  bungeni na Spika wa zamani Justin Muturi kuhusu suala hilo mnamo mwaka wa 2014 kuhusu uteuzi wa aliyekuwa Waziri wa Usalama Joseph Ole Nkaissery.

“Katika uamuzi wake, Spika alisema kuwa afisi ya umma haiwezi kusalia wazi kwa misingi kuwa mshikilizi wake amependekezwa kwa uteuzi katika wadhifa mwingine. Kwa hivyo, marehemu Nkaissery aliendelea kuhudumu kama Mbunge wa Kajiado ya Kati hadi pale Bunge lilipoidhinisha uteuzi wake kutoa nafasi kwa rais kuteuzi rasmi kwa wadhifa mpya wa uwazi,” Bi Nderitu akaeleza.

“Kwa hivyo, nilifahamu hili nilipowasilisha barua ya kuomba nafasi hii. Nilijua kwamba nitajiuzulu rasmi baada ya kukamilisha kwa mchakato mrefu wa uteuzi,” akaongeza.

Bi Nderitu alitoa ufafanuzi huo baada ya Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo kusema kuwa baadhi ya Wakenya waliwasilisha memoranda kwa kamati hiyo wakipinga kuidhinishwa kwake kwa misingi kuwa anashikilia wadhifa wa Msajili wa Vyama vya Kisiasa na hivyo ni Afisa Mkuu wa Serikali.

“Tumewasilisha memoranda kadhaa zikipinga uteuzi wake kwa misingi kuwa wakati huu unahudumu kama Msajili wa Vyama vya Kisiasa na hivyo haifai kushindania wadhifa wa kamishna wa IEBC,” Bw Amollo akaeleza.

Makamishna wengine waliokuwa wamefika mbele ya JLAC kufikia Jumamosi saa nane alasiri kupigwa msasa ni aliyekuwa wakili wa chama cha Amani National Congress (ANC) kilichovunjwa Moses Alutalala Mukhwana na wakili Bi Mary Karen Sorobit.