Boniface Kariuki, mchuuzi aliyepigwa risasi kichwani na polisi ameaga dunia, familia yasema
BONIFACE Kariuki, mchuuzi aliyepigwa risasi kichwani wakati wa maandamano ya kupinga ukatili wa polisi Juni 17, 2025 ameaga dunia, familia sasa yathibitisha.
Msemaji wa familia Emily Wanjira alisema kupitia mawasiliano ya simu kwamba Boniface alikata roho leo (Juni 30, 2025) 3.15pm baada ya kuwa mahututi tangu alipokimbizwa hospitalini na Wasamaria Wema baada ya kupigwa risasi kichwani na polisi wakati wa maandamano ya Juni 17, 2025.
Jana Jumapili, familia hiyo ilikuwa imesema kwamba madaktari waliwaambia alikuwa amekufa ubongo; hivyo kilichokuwa kinapiga ni moyo pekee kwa usaidizi wa mashine.
“Sheria za Kenya haziruhusu mashine zizimwe, kile tunachoweza kufanya sasa ni kusubiri tu hatima yake. Bili ya hospitali ni karibu Sh3 milioni na sasa tunatoa wito kwa wahisani waingilie watusaidie, akili ya mtu ikibainika imekufa, sasa hapo hakuna matumaini,” aliongeza Bi Wanjiru akiwa amejaa masikitiko Jumapili.
Kwa kawaida, ubongo wa mtu ukifa, basi hiyo ina maana kuwa shughuli zote za mwili zimelemazwa na ni kama tu anayerejelewa ashakumbatia mauti.
Bi Wanjira alisema kuwa mnamo Alhamisi wiki jana, waliambiwa kuwa bado kulikuwa na kipande cha risasi ambacho kilikuwa kimekwama kwenye ubongo wa Kariuki.
Bw Kariuki alikuwa akiuza barakao kabla ya kujipata kwenye tafrani kati ya waandamanaji na polisi ambapo alipigwa risasi.