Habari

Bunge la Kaunti ya Bomet kuchunguza madai daktari alibaka mama mjamzito

Na VITALIS KIMUTAI February 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BUNGE la Kaunti ya Bomet limetwikwa jukumu la kuchunguza kisa ambapo daktari anadaiwa kumbaka mwanamke mjamzito.

Idara ya Uchunguzi wa Uhalifu (DCI) ilichukua usukani kuhusu suala hilo kutoka kwa polisi wa kawaida Jumanne kutokana na shinikizo za wadau waliotaka suala hilo kutatuliwa kikamilifu.

Maswali yameibuka kuhusu ni kwa nini hatua haikuchukuliwa kuhusu kisa hicho kinachosemekana kuripotiwa Januari 19, 2026, huku mamlaka ikionekana kugutushwa na ripoti za vyombo vya habari.

Imeibuka vilevile kwamba baadhi ya maafisa wa serikali walijaribu kuzima suala hilo lilipozuka, kukiwa na juhudi za kumshawishi mlalamishi kuondoa malalamishi.

Mwanamke huyo anadaiwa kudhulumiwa kingono na maafisa wa afya katika Kituo cha Afya cha Chemaner, eneobunge la Bomet Mashariki alipokuwa ameenda kujifungua.

Katika tuko hilo la kusikitisha, mhasiriwa aliyeandamana na jamaa anadaiwa kutendewa ukatili huo katika chumba cha ukaguzi.

Kutokana na masaibu hayo, mhasiriwa alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Longisa ambapo alilazwa na kujifungua kwa njia ya kawaida kabla ya kuruhusiwa kurejea nyumbani.

“Mshukiwa alikamatwa, akaandikisha taarifa na kupewa dhamana ya pesa taslimu, suala hilo linachunguzwa,” akasema Kamanda wa Polisi Bomet Mashariki, Michael Mwenda.

Waziri wa Afya katika Kaunti ya Bomet, Felix Langat, amethibitisha vilevile kwamba tukio hilo la kushtusha linachunguzwa, huku ikiibuka kwamba ilichukua majuma kadhaa na shinikizo kali kutoka kwa wadau kabla ya suala hilo kupiga hatua na utawala wa Kaunti kukiri kuwepo kwa malalamishi hayo.

Spika wa Bunge la Kaunti Cosmas Korir, aliamuru, “Imeagizwa kwamba kamati za Jinsia na Huduma za Kijamii zichunguze madai ya mama mjamzito kubakwa katika Kituo cha Afya cha Chemaner na kuwasilisha ripoti katika muda wa siku saba.”

Hii ilifuatia hoja iliyowasilishwa Jumanne na Diwani wa Chemaner Richard Ruto aliyesema wakazi eneo hilo na wadau mbalimbali wanafuatilia suala hilo kwa makini na ni muhimu kufafanua hali na kuchukua hatua.

“Tukio hilo limeathiri pakubwa kisaikolojia mhasiriwa, familia, wagonjwa na wakazi eneo hilo,” alisema Bw Ruto.

Mwenyekiti wa Kamati ya Afya Stephen Changmorik na mwenzake wa Jinsia Japeth Cheruiyot, wameahidi kufanya hima kukamilisha uchunguzi.