DCI wasema wamefanikiwa kulemaza genge la utapeli mitandaoni
GENGE ambalo limekuwa likiwalaghai watu hela zao kupitia uhalifu wa kimtandaoni hatimaye limemalizwa na makachero kutoka Idara ya Upelelezi Nchini (DCI).
Ikifahamika kama matapeli wa simu ambao walikita kambi Mulot, Kaunti ya Bomet, genge hilo linaaminika limewapora Wakenya kutoka maeneo ya Nakuru, Nyahururu na miji ya karibu zaidi ya Sh11.8 milioni.
Makachero walisema kuwa genge hilo liliwalenga wale ambao wamestaafu hasa wanawake baada tu ya pesa zao za pensheni kuingia kwenye akaunti zao.
Wafanyabiashara pia walikuwa wakilengwa na wahalifu hao ambao walitumia ujuzi wao wa teknolojia kuingia kwenye akaunti zao za benki kwa kuwahadaa wawape habari au maelezo muhimu kisha kuwapora hela zao.
Baada ya kuvuna wasikopanda, wahalifu hao walikuwa wakitupa laini zao za simu na kuzima simu ili wasifikiwe. Hata hivyo, kosa la mshukiwa mmoja kwenye genge hilo lilichangia kukamatwa kwao.
Mshukiwa huyo alitumia simu iliyoibwa na akakosa kuizima na hilo liliwawezesha makachero kumsaka na wakampata kwenye maficho Nyali, Kaunti ya Mombasa.
Washukiwa sita walikamatwa kwenye nyumba moja ya kifahari mtaani humo huku simu 19 zikipatikana, laini kadhaa za simu za kampuni za Safaricom, Airtel, Telkom na MTN Uganda pamoja na kitabu cha umiliki gari lenye majina ya waliotapeliwa.
Washukiwa waliokamatwa ni Fortune Muthina Kinyanzui, Ruel Kipkoech, Laban Kipkirui, Weldon Kipyegon, Towet Kipkorir na Kelvin Kipkoech.
Kwa mujibu wa Mkuu wa DCI Mohamed Amin, genge hilo lilitumia teknolojia ambapo waliolengwa walifikiria wanapokea simu kutoka kwa maajenti wa benki ambako wana akaunti.
“Wengi bila kujua walikuwa wakisema nambari zao za siri kisha kugutuka akaunti zao zimesafishwa kwa hela kuhamishwa,” akasema Bw Amin.
Washukiwa hao wamezuiliwa katika kituo cha polisi cha Capitol Hill huku uchunguzi ukiendelea wa kuwaandama washukiwa zaidi wa genge hilo linaloaminika lina matawi yake miji mbalimbali nchini.
Haya yanafanyika wengi walitapeliwa wakijitokeza na kueleza masaibu yao mmoja wao akiwa mfanyabiashara Nyahururu ambaye alipoteza Sh3.4 milioni mnamo Januari 17, 2025.