Habari

Diwani na washukiwa watatu wanaohusishwa na utekaji nyara wa Koimburi waachiliwa kwa dhamana

Na RICHARD MUNGUTI May 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

DIWANI wa wadi ya Kanyenyaini Kaunti ya Kiambu, Grace Nduta Wairimu aliyekamatwa pamoja na watu wengine wanne kuhusiana na utekaji nyara wa Mbunge wa Juja George Koimburi wameachiiliwa kwa dhamana ya Sh1milioni.

Pia Nduta pamoja na Peter Kiratu Mbari, David Macharia Gatana na Cyrus Kiiru walipewa dhamana ya pesa tasilimu Sh300,000 wakishindwa kupata dhamana.

Wote wameachiliwa baada ya kulipa kiasi hicho cha pesa.

Akiwaachilia kwa dhamana hakimu mwandamizi Carolyne Nyaguthii Mugo aliwaamuru washukiwa hao wawe wakipiga ripoti kwa afisa anayechunguza kesi hiyo katika muda wa siku 15 zijazo.

Bi Mugo pia aliwaagiza washukiwa hao wasivuruge uchunguzi kwa kuzugumza na mashahidi.

Bi Mugo alitoa maagizo hayo alipotupilia mbali  ombi la  mkurugenzi wa mashtaka ya umma (DPP) Renson Ingonga la kuwazuilia washukiwa hao kwa siku 15 kukamilisha uchunguzi.

Kupitia kwa kiongozi wa mashtaka Ingonga aliomba washukiwa hao wazuiliwe rumande kuwezesha polisi kukamilisha uchunguzi.

Hakimu alielezwa kwamba washukiwa hao wanachunguzwa kwa kwa makossa ya kumteka nyara Koimburi kwa lengo la kumuua.

Pia korti ilielezwa washukiwa hao wanachunguzwa kwa makosa ya kuzua vurugu.

Hakimu alifahamishwa usalama wa washukiwa hao uko hatarini kwa vile “wananchi wameeleza wasi wasi wao na mahangaiko makuwa kufuatia kutoweka kwa Mbunge wao.”

Katika uamuzi wake hakimu alisema ombi la DPP halina mashiko kisheria na kuitupilia mbali.

“Kama washukiwa hawa wangelitishwa wangelikuwa wamepiga ripoti kwa polisi,” alisema Bi Mugo.

Mahakama ilikubaliana na mawasilisho ya wakili Kiragu Wathuta kwamba dhamana ni haki ya washukiwa “na hakuna sababu zozote zilizotolewa na DPP kuwezesha mahakama kuwazuilia uchunguzi ukiendelea.”

Hakimu alisema polisi wanaweza kuendelea na uchunguzi wa simu za washukiwa hao wane wakiwa nje kwa dhamana.

Bi Mugo aliwaamuru washukiwa hao wawe wakipiga ripoti kwa afisa anayechunguza kesi hiyo.

Mahakama ilisema polisi hawajaandikisha taarifa kutoka kwa Bw Koimburi anayeendelea kupata matibabu katika Karen Hospital.

Mbunge huyo alitekwa nyara na akapatikana katika shamba la kahawa kaunti ya Kirinyaga akiwa na majeraha.

Washukiwa hao watafika kortini tena Juni 17,2025 mkurugenzi wa mashtaka ya umma (DPP) aeleze mahakama ikiwa amekamilisha uchunguzi wa kesi hiyo.

Kutoweka kwa Koimburi kulizua hisia kali katika ulingo wa kisiasa.