Habari

DPP kukata rufaa uamuzi ulioachilia huru Rose Njeri

Na RICHARD MUNGUTI June 23rd, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MKURUGENZI wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga amesema atakata rufaa kupinga uamuzi wa kutamatisha kesi ya matumizi mabaya ya mitambo ya mawasiliano dhidi ya mwanaharakati Rose Njeri.

Hatua hii ya DPP inamaanisha bado Njeri hayuko huru kabisa kwa vile huenda akashtakiwa tena.

Bw Ingonga alisema hakuridhishwa na uamuzi wa Hakimu Mwandamizi wa Mahakama ya Milimani Geoffrey Onsarigo wa kufutilia mbali kesi aliyoshtakiwa Njeri akisema “hakuna makosa aliyotenda.”

Kupitia wakili Danstan Omari, Bw Ingonga alisema atakata rufaa kurejesha kesi dhidi ya Njeri akisema “mahakama ilitupia kipengee kisichofaa kisheria kumwachilia mwanaharakati huyu.”

Bw Onsarigo, aliyemwachilia Njeri alisema “Kifungu cha Sheria nambari 16 ya Sheria za Uhalifu wa Mitandao hakikufichua makosa aliyofanya mwanaharakati huyu.”

Hakimu huyo alikubaliana na utetezi wa mawakili Kalonzo Musyoka, aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, mawakili Eric Theuri na Kibe Mungai kwamba “mmoja hawezi kushtakiwa kwa kutekeleza haki yake ya kisheria na Katiba.”

Mawakili hao walieleza mahakama Njeri aliwaalika Wakenya kutoa maoni kuhusu Mswada wa Fedha wa 2025/2026 na hakuna “makosa aliyofanya kwa vile alitumia mtandao wa bunge iliyofungua kupokea maoni ya wananchi kuhusu sheria hii ya fedha.”

Bw Omari alisema Bw Ingonga ameeleweka vibaya katika habari zilizochapishwa na baadhi ya vyombo vya habari  na mitandao ya kijamii kwamba haelewi sheria za uhalifu wa kimitandao.