Duale: Zaidi ya nusu ya hospitali zinazolaghai SHA zinamilikiwa na Waislamu
WAZIRI wa Afya Aden Duale amesema zaidi ya nusu za hospitali na vituo vya afya vinavyoshiriki ulaghai katika Mamlaka ya Bima ya Kitaifa (SHA) zinamilikiwa na Waislamu.
Kutokana na hilo, Bw Duale ametaka wenye hospitali hizo wazingatie dini na maadili katika masuala ya pesa za umma.
Kwa mujibu wa waziri huyo, asilimia 55 ya vituo vya afya 1,120 ambavyo vilifungwa kutokana na ulaghai wa SHA, vinamilikiwa na Waislamu.
Aliongeza kuwa wizara yake inapanga kufunga hospitali na vituo vya afya vingine wiki hii ambapo alifichua asilimia 60 zinamilikiwa na Waislamu.
“Mnafaa mhakikishe mnawapa watoto wenu malezi mazuri kwa pesa halali,” akasema.
Alikuwa akiongea Jumapili wakati wa iftar iliyoandaliwa na Chama cha Madaktari na Wahudumu wa Kimatibabu Waislamu (KAMMP), hafla iliyoandaliwa jijini Nairobi.
Bw Duale alisema yeye pamoja na Mwenyekiti wa SHA Dkt Abdi Mohamed, watahakikisha wanaendeleza maadili katika kazi yao.
“Afya si taaluma tu bali ni imani tumewekewa. Nawaomba wataalamu Waislamu wazingatie maadili, wajiheshimu na wajikite katika kutoa huduma bora,” akasema.
Mnamo Februari 26, Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) iliidhinisha kushtakiwa kwa vituo vinane vya kiafya kwa kulaghai SHA.
Vituo hivyo vinatoka Kaunti ya Mandera na vilisajiliwa kati ya Januari na Februari 2025 mwezi mmoja tu baada ya SHA kuanza kujumuisha hospitali kwenye mtandao wake.
Hospitali hizo na vituo vya afya ni Danaba, Kamishawa, Kaafi, Mama Narbeel, Alati, Julun, Adfaal na Dimtu.
Katibu Mkuu wa KAMMP Dkt Abdallah Bajaber aliwakashifu wamiliki wa hospitali hizo kwa kuchafua jina la Waislamu, akisema maadili hayafai kulegezwa.
“Wala msile mali ya mtu mwengine kiharamu au kuituma kama hongo kwa watawala ndipo ule mali ya watu kwenye dhambi huku ukijua ni kinyume cha sheria,” akasema Dkt Bajaber akinukuu aya ya Quran 2.188.
Katibu huyo alikanusha dhana ya baadhi ya Waislamu kuwa kula pesa za SHA si haramu eti kwa sababu ni pesa ya serikali.