Familia ya Ojwang yasihi Wakenya wakome kuishambulia mitandaoni
FAMILIA ya marehemu mwalimu wa shule ya upili na mwanablogu, Albert Ojwang aliyeuawa akiwa seli ya polisi, imeomba Wakenya wakome kuishambulia mtandaoni baada ya kufichua kwamba ilipokea msaada wa kifedha kutoka kwa Rais William Ruto na kiongozi wa ODM Raila Odinga.
Baba yake Albert, Meshack Ojwang, alithibitisha kuwa familia hiyo ilipokea jumla ya Sh3 milioni kutoka kwa viongozi hao wawili waliotoa rambirambi zao.
Familia ilikabidhiwa fedha hizo ilipotembelewa na Gavana wa Homa Bay, Gladys Wanga, pamoja na Mbunge wa Kabondo Kasipul, Eve Obara, Juni 16, 2025.
Hata hivyo, mara tu Bw Ojwang alipotangaza msaada huo hadharani, alikosolewa vikali mitandaoni, hasa kwa kupokea pesa kutoka kwa Rais Ruto, ambaye wengi wanalaumu serikali yake kwa kuhusika na kifo cha kikatili cha mwanawe.
“Haya mashambulizi si ya haki wala hayana msingi. Wakenya wengi wametuunga mkono katika kipindi hiki kigumu mno; msaada huu haukuwa tofauti.”
“Ni sehemu ya utamaduni wetu wa Kiafrika, hasa wa Wajaluo, kupokea msaada kutoka kwa waombolezaji. Mchango huu ulitokana na huruma na upendo, si siasa, na si jambo la kujadiliwa hadharani,” alisema mjomba wa Ojwang, Herman Opiyo.
Aliongeza kuwa familia inayoomboleza mara nyingi huchukua hatua za haraka na haipaswi kuhukumiwa kwa namna inavyoshughulikia hali inayoikumba.
“Hatuwezi kuwafukuza watu wanaokuja kutufariji. Tusingeweza pia kuficha msaada ambao umetangazwa hadharani. Tulikubali kwa moyo ule ule ambao tungepata kutoka kwa wafadhili wengine,” alisema.
Familia hiyo, ambayo bado inakumbwa na huzuni, pia imepata pigo jingine baada ya watu wasiojulikana kuiba fedha kutoka kwa simu ya baba ya Ojwang.
Kulingana na Bw Opiyo, ingawa kiasi kamili cha pesa kilichoibiwa hakijajulikana, rekodi zinaonyesha kuwa pesa zilihamishwa kutoka kwa akaunti hiyo kwenda kwa nambari isiyojulikana.
Fedha hizo zilihusisha akiba ya kibinafsi na michango kutoka kwa Wakenya kupitia mpango wa msaada wa “Sisi kwa Sisi” ulioanzishwa na chale au mchekeshaji Eric Omondi.
Bw Omondi, aliyetoa video ya kuomba msaada kwa ajili ya familia ya Ojwang, alieleza kuwa nambari kadhaa za simu zilitumika kupokea michango baada ya nambari ya kwanza kufikia kiwango cha juu cha Sh500,000.
“Aligundua kuwa kuna tatizo wakati hakuweza kupiga wala kupokea simu. Ilikuwa kana kwamba mtu alidukua simu yake,” alisema.
Kisa hicho kilitokea wakati babake Ojwang alirejea nyumbani asubuhi ya Jumamosi kuhudhuria mazishi ya shemeji yake.
Bw Opiyo hakuweza kuthibitisha iwapo suala hilo liliripotiwa rasmi kwa polisi, lakini alisema anaamini kuwa rekodi zitafichua kilichotokea.
Katika pigo jingine, Bw Opiyo alifichua kuwa watu wengine wamejaribu kurudisha michango waliyotoa awali.
“Hili linatuumiza sana na ni la kudhalilisha. Tuko katika maombolezo. Kuchangia halafu kurudisha pesa ni sawa na dhihaka na kutoheshimu huzuni yetu,” alisema.
Marehemu Ojwang atazikwa Julai 4 2025 katika boma la wazazi wake kijijini Kakoth, Kaunti ya Homa Bay.
Tarehe hiyo ya mazishi ilikubaliwa wakati wa mkutano wa familia uliofanyika mwishoni mwa wiki.
Ibada ya mazishi, itakayoongozwa na askofu kutoka Kanisa la Baptist, itafanyika katika Shule ya Msingi ya Nyawango kabla ya mwili kupelekwa nyumbani kwao kwa ajili ya mazishi.