Habari

Familia ya Ojwang yataka ilindwe ikisaka haki kwa mpendwa wao

Na ERIC MATARA June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

FAMILIA ya mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang’, anayedaiwa kuuawa akizuiliwa na polisi katika kituo cha Polisi cha Nairobi Central, inataka serikali iwape ulinzi wa kutosha wanapofuatilia haki kwa mpendwa wao.

Wakili wa familia, Julius Juma, aliyekuwa akizungumza katika kipindi cha Fixing the Nation, katika runinga ya NTV jana asubuhi, alisema wanahitaji kulindwa wasidhuriwe kutokana na uzito wa suala hilo.

“Tunataka tuhakikishiwe usalama wetu tunapopigania haki ya Albert Ojwang’. Kila mtu aliye upande wa familia, mimi nikiwa mmoja wao, tunajihisi tuko hatarini,” alisema Bw Juma.

“Ninaomba ulinzi kwa familia na mimi binafsi, kwa sababu hatujui hasa tunakabiliana na nani katika harakati hizi za kutafuta haki,” aliongeza.

Wakili huyo pia alibainisha kuwa, wasiwasi mkubwa wa familia ni uwezekano wa kuingiliwa kwa uchunguzi na mashahidi.

“Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) kwa sasa inaendelea kuwahoji mashahidi walio katika vituo vya polisi Nairobi na maeneo jirani, na hofu yetu kuu ni kuingiliwa kwa ushahidi na mchakato wa uchunguzi,” alisema Juma.

“Natoa wito kwa uchunguzi kuwa wa uwazi. Ushahidi wote unapaswa kuhifadhiwa na pasiwepo na kuingiliwa kwa uchunguzi au mashahidi. Idara za uchunguzi zinapaswa kufanya kazi yao bila shinikizo au maagizo kutoka nje,” aliongeza.

Wito huo wa wakili kuhusu ulinzi ulitolewa huku afisa wa polisi katika kituo cha Nairobi Central, aliyekuwa zamu usiku wa mauaji ya kikatili ya Ojwang’, akidai maafisa wa ngazi za juu walihusika na kupanga ateswe.

Konstebo James Mukhwana, aliyekuwa mlinzi wa seli, katika ushahidi wake kwa IPOA, anasema Mkuu wa Kituo cha Polisi (OCS), Samson Talaam, alimjulisha kuhusu kuwasili kwa Ojwang’ na kumuagiza apange wafungwa wengine kazi ya kumpiga.