Habari

Gachagua aandamwa kuhusu wosia wa urithi wa ndugu yake marehemu

Na MWANGI MUIRURI Na ELVIS ONDIEKI March 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WOSIA uliosifiwa kama mojawapo ya bora zaidi kuwahi kuandikwa nchini Kenya na aliyekuwa Gavana wa Nyeri, marehemu Nderitu Gachagua, sasa umeibua mzozo mkali wa kifamilia na kisiasa unaomhusisha Rais William Ruto na aliyekuwa Naibu wake Rigathi Gachagua.
Nderitu, kakake Rigathi, alifariki Februari 24, 2017 akipokea matibabu ya saratani ya kongosho katika Hospitali ya Royal Marsden, London.
Wakati wa kifo chake, alikuwa katika mwaka wa tano wa muhula wake wa kwanza kama gavana wa Nyeri.
Aliacha wosia uliotoa mwongozo kuhusu ugavi wa mali yake kwa watu 21, ambao ulitekelezwa 2018.
Wosia huo ulisifiwa na mawakili wengi kwa kufunga mianya ambayo mara nyingi husababisha migogoro ya kifamilia baada ya kifo cha mpendwa.
Rigathi amesema wosia huo hata hufundishwa katika Chuo cha Sheria cha Kenya kutokana na ubora wake.
Kwa mujibu wake, falsafa ya wosia huo ilikuwa kuuza mali yote ya marehemu, kulipa madeni, kisha kugawa fedha zilizobaki kwa waliotajwa kunufaika kulingana na asilimia zilizobainishwa.
Hata hivyo, baadhi ya watu walionufaika sasa wanahoji uhalali wa wosia huo, wakisema ulitiwa saini wakati marehemu alikuwa mgonjwa mahututi.
Katika barua iliyoandikwa kwa Rais Ruto, jamaa watano walidai hali ya Nderitu ilikuwa mbaya kiasi kwamba, hangeweza kuona, kuelewa au kutia saini nyaraka za kisheria.
Katika barua hiyo iliyotiwa saini na Margaret Nyokabi, Susan Kirigo, Mercy Wanjira, Jason Kariuki na Ken Gachagua, waliomba Rais aingilie kati ili kuanzisha uchunguzi huru na kuhakikisha mali iliyodaiwa kuhamishwa kwa njia isiyo halali inarudishwa.
Pia, wanaomba ulinzi dhidi ya vitisho wanavyodai wanakumbana navyo.
Lakini Rigathi alipinga madai hayo vikali, akisema ni njama ya kisiasa inayochochewa na Rais Ruto ili kuharibu jina na hadhi yake kisiasa.
Alidai hakuna kosa lolote lililofanywa katika utekelezaji wa wosia huo.
“Ni miaka tisa tangu afariki. Mbona suala hili linaibuka sasa?” alihoji.
Rigathi alisisitiza kuwa mali yote iliyouzwa iligawiwa wote waliopaswa kunufaika kwa haki, akisema kuwa alipata asilimia tano ya mapato, sawa na baadhi ya ndugu wengine, wakiwemo wake wa marehemu.
Alieleza kuwa waliopata asilimia 10 walipokea takriban Sh50 milioni huku waliopata asilimia tano wakipokea Sh25 milioni baada ya mali kama vile hoteli ya Olive Gardens kuuzwa.
Aidha, alisema wosia huo uliwahusisha wake wawili wa marehemu, watoto wake, pamoja na wanawake wengine waliokuwa sehemu ya maisha yake na watoto wao, pamoja na ndugu na jamaa wengine.
Suala la wosia huo lilijitokeza pia wakati wa mchakato wa kumuondoa Rigathi madarakani mnamo 2024, ambapo alishutumiwa kwa madai ya kubadilisha wosia huo ili kuwanyima baadhi ya waliopaswa kunufaika na urithi. huo.
Hata hivyo, alikanusha madai hayo bungeni, akisema mali hiyo ilisimamiwa kulingana na maagizo ya marehemu.
Kwa upande wao, waliotia saini barua hiyo walisema walikaa kimya kwa muda mrefu kwa heshima na matumaini ya kupata suluhu kifamilia, lakini walilazimika kuzungumza hadharani kutokana na kile walichokitaja kama dhuluma na udanganyifu.
Bw Rigathi aliwataka walalamishi kufuata njia za kisheria badala ya kumhusisha Rais, akisema tayari suala hilo lilishughulikiwa mahakamani na kufungwa kwa makubaliano ya pande zote.
Alidai pia kuwa baadhi ya walalamishi walishawishiwa kisiasa kuibua upya suala hilo, madai ambayo yamekanushwa na mmoja wa wasemaji wa familia, Susan Kirigo, aliyesema hawajawahi kukutana na Rais moja kwa moja.
Kirigo alisema familia ina matumaini kuwa Rais atasikiliza kilio chao na kusaidia kuhakikisha haki inapatikana.