Habari

Gachagua sasa ataka fidia kwa kutimuliwa afisini, asema hataki kurudishiwa kiti

Na SAM KIPLAGAT May 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Naibu Rais, Rigathi Gachagua, hatalazimisha arejeshwe ofisini  na badala yake anasema ata omba mahakama kumlipa fidia kwa kufutwa kazi kinyume na sheria, pamoja na marupurupu yote ambayo angepokea iwapo angebaki kazini hadi mwisho wa muhula wake wa miaka mitano.

Gachagua aliondolewa ofisini baada ya kuhudumu kwa miezi 24 pekee, huku akipokea mshahara wa takriban Sh1.2 milioni kwa mwezi, ukiwemo mshahara wa msingi wa Sh736,313,  marupurupu ya nyumba ya Sh300,000, na  ya usafiri miongoni mwa marupurupu mengine.

Kulingana na Sheria ya Marupurupu ya Kustaafu kwa Naibu Rais na Maafisa Wengine wa Kuteuliwa (2015), anastahili pensheni ya kila mwezi sawa na asilimia 80 ya mshahara wake wa mwisho.

Katika kikao cha Alhamisi mbele ya jopo la majaji watatu, Eric Ogola, Anthony Mrima na Dkt Freda Mugambi, wakili wake Paul Muite aliwasilisha ombi la kubadilisha malalamishi yake ya awali ili kuondoa ombi la kurejeshwa kazini.

“Mteja wangu anataka kuweka wazi kwamba hataki kurejeshwa katika wadhifa wa Naibu Rais wa Jamhuri ya Kenya,” alisema Muite.

Badala yake, Gachagua atapinga vikali uhalali wa kuondolewa kazini  na ataomba mahakama kutupilia mbali hatua ya kumtimua, pamoja na kumlipa malipo yote ya kipindi kilichosalia cha miaka mitano, pamoja na fidia kwa kuharibiwa kwa hadhi na haki zake.

Mnamo Oktoba 8, 2024, Bunge la Kitaifa lilipiga kura  kumuondoa ofisini, na Oktoba 17, Seneti iliidhinisha hoja hiyo kufuatia mashtaka 11 dhidi yake.

Katika kesi yake, Gachagua anadai kuwa mchakato huo haukufuata viwango vya kikatiba vinavyotakiwa na Kifungu cha 145(1) cha Katiba. Pia, anadai kuwa hakupata haki ya kusikilizwa kama inavyotakiwa chini ya Kifungu cha 50(1).

“Mashtaka hayo yaligeuzwa kuwa mashambulizi ya familia yake badala ya uchunguzi wa ukiukaji wa katiba,” alisema.

Kesi hiyo ilicheleweshwa baada ya Gachagua kupinga Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu kwa kuteua majaji kinyume cha sheria. Mahakama ya Rufaa ilikubaliana naye na kuamuru Jaji Mkuu Martha Koome kuteua majaji wapya. Hata hivyo, Jaji Koome aliwateua tena majaji wale wale kuisikiliza.

Kesi hiyo itatajwa tena Julai 18 kwa mwelekeo zaidi. Wakati huohuo, baadhi ya walalamishi wameomba kesi tano ziondolewe kwa kuwa zinashughulikia masuala yanayofanana, lakini mwanaharakati mmoja amepinga hatua hiyo akitaka ziendelee kusikilizwa kikamilifu