Gavana Guyo kujitetea mbele ya maseneta wote badala ya kamati
GAVANA wa Isiolo Abdi Guyo atafika mbele ya maseneta wiki ijayo anapopambana kusalia afisini baada ya kutimuliwa na madiwani wiki jana.
Haya yanafanyika huku masuala ya kisheria yakiibuka kuhusu uhalali wa Seneti kumchunguza gavana huyo. Hii ni kwa sababu kulikuwa na amri ya korti iliyowazuia madiwani kumtimua Bw Guyo.
Seneti itaanza kumsikiza Bw Guyo mnamo Julai 8 na vikao hivyo vitaendelea Julai 9 na Alhamisi Julai 10, 2025.
Uamuzi wa Seneti nzima kusikiza kutimuliwa kwa gavana huyo anayehudumu muhula wake wa kwanza, unatokana na jitihada za kuundwa kwa kamati ya wanachama 11 kugonga mwamba.
Kiranja wa Wengi Boni Khalwale kwa niaba ya Kiongozi wa wengi Aaron Cheruiyot alikuwa amewasilisha hoja ya kubaini iwapo kamati spesheli itasikiza kesi hiyo au itakuwa mbele ya Seneti nzima.
Hata hivyo, Kiongozi wa Wengi Stewart Madzayo ambaye alitarajiwa kuunga hoja hiyo aliipinga na kupisha kusikizwa kwake na maseneta wote.
“Njia ya kamati sasa inatelekezwa na hii ina maana kuwa pendekezo la kumwondoa Gavana wa Isiolo Abdi Guyo kupitia kutimuliwa kwake, sasa litasikizwa na Seneti nzima na si kamati ya Seneti,” akasema Gavana Amason Kingi.
Madiwani, Bw Guyo na wote wanaoshirikishwa katika kumwondoa gavana afisini, walikuwa wamepewa hadi Juni 27 (Ijumaa iliyopita) kuwasilisha stakabadhi na ushahidi.
Mchakato wa Seneti unaendelea wakati ambapo Jaji wa Mahakama ya Isiolo Heston Nyaga alikuwa ameukataa na kutoa amri ya kuuzuia.
Jaji Nyaga alimpata Spika wa Bunge la Kaunti Mohamed Roba na hatia ya kupuuza korti na akamwaamrisha afike mbele yake kortini Jumatatu.
Jaji huyo alikuwa amesema kuwa amri aliyokuwa ametoa mnamo Juni 16 ya kuzuia Bunge la Kaunti kuendelea na mchakato wa kumbandua gavana mamlakani bado ipo.
Alionya kuwa amri hiyo ikikiukwa, bado mchakato wa kumtimua Bw Guyo hautakuwa na mashiko yoyote.
“Amri hiyo itabaki hadi pale iwekwe kando au kuangaziwa na mahakama hii, korti nyingine au Mahakama ya Rufaa,” akasema Jaji Nyaga.
Licha ya amri ya korti, madiwani 16 kati ya 18 walipiga kura mnamo Alhamisi wiki jana na kumbandua Bw Guyo.
Gavana ambaye madiwani walikuwa wamemwalika ajitetee kuhusu madai yaliyokuwa yamemkabili, alikanusha vikali kuwa aliupata mwaliko wowote kutoka kwa Bunge la Kaunti.
Mnamo Ijumaa wiki jana, mawakili wa Bw Guyo, wakiongozwa na Eric Theuri na Elias Mutuma, waliwasilisha kesi dhidi ya spika na karani kwa kupuuza amri ya korti.
Jaji Nyaga, aliamrisha wawili hao wafike mbele yake Juni 30 ili kujibu madai hayo.