Habari

Gavana motoni kwa kuwadhalilisha wanawake wa Taita

Na LUCY MKANYIKA June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WANAWAKE katika Kaunti ya Taita Taveta wamemtaka Gavana Andrew Mwadime kuomba msamaha kwa matamshi ya kuwadhalilisha.

Hii ni baada ya Gavana Mwadime kudai kuwa wanawake warefu katika kaunti hiyo wameolewa nje ya gatuzi na kwamba waliosalia ni wafupi ambao ni wasumbufu.
Gavana alitoa matashi hayo wiki jana wakati wa kikao cha maafisa wa serikali ya kaunti na Kamati ya Seneti kuhusu Uhasibu wa Fedha za Umma (CPAC) inayoongozwa na Seneta Moses Kajwang’.
“Sisi kama kaunti tuna shida nyingi sana. Kilichosalia sasa ni watu wanakuja, wanaoa wasichana wetu warembo na wanatuachia wale wafupi. Tunauliza Seneti itusaidie,” alisema kwenye kikao hicho.
Alipoulizwa na Seneta Kajwang’ ikiwa wanawake wafupi si warembo, Bw Mwadime alisema wao huwa wana ugomvi na husumbua.
Sasa wanawake wakiongozwa na shirika la Sauti ya Wanawake wanasema gavana aliwakosea heshima wanawake wote wa eneo hilo kwa kudai wale wafupi wanapenda ugomvi.
Mwenyekiti wa shirika hilo Bi Lydia Mwamberi alipuuzilia mbali madai kuwa Gavana alikuwa akifanya mzaha alipotoa matamshi hayo, akisema wanawake kote vijijini wanalalamika kwamba aliwadharau.
“Ufupi au urefu ni maumbile ya mtu. Mbona alitaja wanawake na sio wanaume? Pia kuna wanaume wafupi na wanaoa wanawake warefu,” akahoji.
Bi Mwamberi alisema walishangazwa na hatua ya gavana kudhalilisha wanawake mbele ya Seneti badala ya kujadili kuhusu masuala ya maendeleo na changamoto zinazokumba kaunti yao.
Aliapa kuwa iwapo Gavana Mwadime hataomba msamaha basi wanawake wa eneo hilo wataandamana hadi atakapotoa radhi hiyo.
Ni msimamo ulioshikiliwa pia na Bi Makrina Mwamburi akisema kuwa walighadhabishwa na matamshi ya kiongozi wao na kwamba yameshusha hadhi ya wanawake eneo hilo.
“Tunataka kujua kutoka kwake maana ya maneno aliyosema. Kwa nini alitudharau namna hii? Sisi ndio tulimpa kura!” aliwaka.
Naye Bi Mary Sau alishangaa kwa nini Bw Mwadime bado anasita kuomba msamaha.
“Gavana ana mke na pia baadhi ya wafanyakazi wake ni wafupi. Matamshi hayo yametukasirisha sana. Asipoomba msamaha tutamwadhibu debeni katika uchaguzi mkuu ujao,” akasema.