Gen Z Billy Mwangi aliyetekwa na kuzuiliwa aweka jicho kwa useneta wa Embu 2027
GEN Z mwenye umri wa miaka 26 ambaye alipata umaarufu baada ya kutekwa nyara na maafisa wa usalama wa serikali na kuzuiliwa kwa zaidi ya wiki mbili bila mawasiliano, ametangaza nia ya kuwania kiti cha useneta Kaunti ya Embu katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.
Bw Mwangi alisema kwenye mahojiano kwamba kuingia kwake katika siasa kunachochewa na hamu ya kuonyesha kuwa kizazi cha Gen Z kinaweza kuongoza kwa uadilifu na kuhakikisha utawala bora.
Bw Mwangi ni mwanafunzi wa mwaka wa nne katika chuo kikuu na anasomea shahada ya Uhalifu na Usimamizi wa Usalama.
Ameeleza kuwa amedhamiria kushinda kiti hicho na kuwa sauti ya vijana ambao, kwa maoni yake, hawawakilishwi ipasavyo.
“Naamini kuwa kizazi cha Gen Z hakina viongozi wa kueleweka, na kinahitaji mtu jasiri na mwenye msimamo wa kuongoza na kutetea haki zao kwa nguvu zote,” alisema Jumanne wakati wa mahojiano.
Licha ya kuwa mpole, Bw Mwangi ni jasiri, na ameahidi kusukuma kupitishwa kwa sheria zitakazolinda maisha ya vijana na kuwawezesha kiuchumi iwapo atachaguliwa.
“Kwa sasa hakuna sheria madhubuti zinazolinda vijana, ndiyo maana wanauawa wanapotetea haki zao,” alisema.
Aliendelea: “Pia tunahitaji sheria zinawezesha ujasiriamali wa vijana kwani zilizopo hazishughulikii ipasavyo masuala ya ufadhili wa miradi ya vijana. Kuna haja ya kutofautisha kati ya vikundi vya vijana na watu binafsi, jambo ambalo halipo katika mifumo ya sasa ya ufadhili.”
Alipoulizwa kama vijana wa Gen Z wamevuka mipaka katika kuikosoa serikali, Bw Mwangi alisema hakuna kosa lolote katika kuikosoa serikali.
“Vijana wana haki ya kutoa maoni yao kuhusu makosa ya serikali ilimradi hawahusiki na vurugu wala uharibifu wa mali. Gen Z hawafai kuogopa kutumia haki yao ya kujieleza lakini maandamano yao yafanyike kwa amani,” alieleza.
Bw Mwangi alitekwa nyara Desemba 21 mwaka jana mjini Embu akisubiri kunyolewa.
Maafisa wa usalama waliokuwa wakiendesha gari la Double Cabin walifika dukani humo, wakamkamata Bw Mwangi na kumbeba kwa nguvu ndani ya gari hilo.
“Nilizuiliwa kwa siku 17 bila mawasiliano na nilipitia mateso makali mikononi mwa watekaji. Hadi leo bado sijapona kiakili na kisaikolojia, maana sijawahi kuelezwa kosa langu. Katika siku zijazo, nitadai fidia pamoja na wenzangu waliopitia mateso kama yangu,” alisema.
Hata hivyo, alisema amewasamehe waliomteka, japo hatasahau mateso aliyopitia.