Amina: ‘Tutam’ ipo ukitujengea uwanja wa ndege Malindi
MBUNGE wa Malindi, Bi Amina Mnyazi, amemwomba Rais William Ruto achukue hatua ili kuharakisha upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Malindi.
Upanuzi huo ambao ulianza kupangwa karibu miaka 15 iliyopita haujapiga hatua kwa sababu ya changamoto mbalimbali ikiwemo fidia kwa wenye ardhi zinazolengwa.
Hata hivyo, Bi Mnyazi alisema tatizo kuu linasababishwa na matapeli walioingilia mpango huo hadi kuukwamisha.
“Tukipata upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Malindi, hata usirudi kufanya kampeni huku maanake sisi wenyewe tutakufanyia. Huu uwanja kuna matapeli watatu kutoka Nairobi ambao wanatatiza mambo hapa. Niite afisini kwako nitakwambia kila kitu,” Bi Mnyazi akasema.
Upanuzi umenuiwa kuwezesha uwanja huo wa ndege kufikia kiwango cha kimataifa, ili kiweze kutumiwa na ndege kubwa zaidi.
Endapo mradi huo utatekelezwa kikamilifu, utachangia kuboresha sekta ya utalii ambayo ni tegemeo kubwa la kiuchumi katika Kaunti ya Kilifi, kwa kuwezesha wageni kusafiri moja kwa moja bila kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Moi mjini Mombasa au ule wa Jomo Kenyatta, Nairobi.
Bi Mnyazi alikuwa akizungumza katika mkutano wa hadhara mjini Malindi, ambao ulihudhuriwa na Rais pamoja na wanasiasa wengine kutoka Pwani.
Rais alikuwa katika Kaunti ya Kilifi kuzindua mpango wa kitaifa wa kuwezesha vijana, almaarufu kama NYOTA, ambao unafadhiliwa na Benki ya Dunia.
Wanasiasa waliohutubia umati, wakiwemo Waziri wa Madini na Uchumi wa Baharini, Bw Hassan Joho, na Spika wa Seneti, Bw Amason Kingi, walishikilia msimamo kwamba Pwani inastahili kumuunga mkono Rais Ruto kwa awamu ya pili ya uongozi ifikapo 2027.
Bw Joho alieleza kuwa, kuna mafanikio mengi yameonekana katika ukanda huo kupitia juhudi za serikali hasa katika sekta ya uvuvi.
Aliorodhesha masuala kama vile ujenzi wa bandari za samaki na uimarishaji usalama baharini kama mifano ya hatua zilizochangia kusaidia wavuvi.
Hata hivyo, baadhi ya viongozi walimkumbusha Rais kuhusu changamoto ya umiliki wa ardhi, wakisema wakazi wengi Pwani bado hawana hatimiliki za ardhi na hii huwaweka hatarini kufurushwa kutoka kwa makao yao na mabwanyenye.
Walirai wananchi wajitenge na wanasiasa wanaoeneza ukabila unaoweza kugawanya taifa kuelekea kwa Uchaguzi Mkuu ujao.