Gavana Andrew Mwadime ‘Wakujaa’ ataka Taita Taveta iwe kitovu cha viwanda
GAVANA wa Taita Taveta, Bw Andrew Mwadime, ametangaza mpango wa kuifanya kaunti hiyo kuwa kitovu cha viwanda kupitia uongezaji thamani wa madini, uzalishaji bidhaa na uchimbaji wa rasilimali asili.
Akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Ranchi ya Ndara B uliofanyika Gimba, gavana huyo alisema hatima ya maendeleo kwa wakazi wa Taita Taveta inategemea jinsi watakavyotumia rasilimali za ardhi na madini.
Mwadime alitaka wanachama wa Ranchi ya Ndara B kuiga mfano wa wenzao wa Mbulia na Kishushe ambazo zimekuwa zikishirikiana na utawala wake kufungua thamani ya madini.
Gavana huyo alieleza kuwa, katika kipindi cha miaka mitatu ofisini, serikali yake imeboresha taratibu za ushirikishwaji wa wawekezaji na kuunda mazingira thabiti na yenye uwazi, hatua iliyowezesha kuanzishwa kwa kiwanda cha kwanza kikubwa cha kuchakata madini katika kaunti hiyo.
Alitaja uwekezaji wa Sh11 bilioni wa kiwanda cha kusindika madini ya chuma kilichojengwa Manga, Wadi ya Ngolia, Voi, na kampuni ya Devki kama hatua muhimu kwa ukuaji wa viwanda, ajira kwa vijana, na kuimarisha uchumi wa eneo hilo.
“Kuendeleza viwanda si ndoto isiyoweza kutimia. Inawezekana kupitia ushirikiano, uwazi, na kuweka maslahi ya jamii mbele,” alisema gavana huyo.