Habari za Kaunti

Jinsi operesheni dhidi ya washukiwa watatu wa wizi ilivyoendeshwa

May 23rd, 2024 2 min read

NA SAMMY KIMATU

KULIKUWA na sarakasi Jumatano asubuhi wakati wa tukio la uhalifu ambapo watu watatu wanaoshukiwa kuwa majambazi walihusika katika ufyatulianaji risasi na polisi.

Kulingana na mkuu wa polisi wa Makadara Bi Judith Nyongesa washukiwa hao wanadaiwa kuwaibia wananchi pesa na simu za rununu walipokuwa wakielekea kazini.

Kulingana na ripoti za polisi, washukiwa hao walikuwa wakinyang’anya raia pesa, simu na mali mkabala wa barabara zenye shughuli nyingi zikiwemo Barabara ya Lusaka, Barabara ya Enterprise na barabara ya Dunga miongoni mwa barabara nyingine katika eneo la Industrial Area.

“Operesheni iliendeshwa na maofisa kutoka kituo cha polisi cha Industrial Area na timu ya Mike Sierra, wakiongozwa na Divpol Makadara na Stapol Indo-Area, ambao walipata taarifa kutoka kwa wananchi waliporwa wakiripoti kwao kuhusu uhalifu wa kunyang’anywa simu za mkononi na pesa huku wakichomolewa na kuelekezewa bastola,” Bi Nyongesa alisema.

Mkuu wa Polisi eneo la Makadara, Bi Judith Nyongesa akiwa katika ofisi yake mnamo Mei 21, 2024. PICHA | SAMMY KIMATU

Majira ya saa moja asubuhi jana timu ya makadara (SPIV) iliwaona washukiwa watatu kando ya Barabara ya Lusaka wakiwa kwenye pikipiki aina ya Boxer KMFG 753 Q ilio na tangi nyeusi.

Walimpora Bw Benard Mutua Mbalu mwenye umri wa miaka 23 alipokuwa akielekea kwenye mahojiano ya kutafuta kazi katika kampuni ya Davis na Shallif.

Mara tu aliponyang’anywa simu yake ya mkononi aina ya Samsung A10 kwa mtutu wa bunduki na kuachwa hoi, mara moja aliwafahamisha maafisa hao ambao walichukua hatua mara moja.

Wapelelezi waliwafuata kutoka Barabara ya Lusaka kuelekea barabara ya Dunga ambapo walipata mwathiriwa mwingine akiibiwa.

Walipokaribia Jamii sacco kulizuka makabilaiano makati ya uftatulianaji risasi baada ya washukiwa kugundua polisi walikuwa wakiwaandama.

Milio ya risasi ilitawala kwa muda huku madereva na watembea kwa miguu wakijificha.

Wengine walionekana wakiwa wamelala chini wakiomba Mungu wasije wakauawa au wakapatwa na risasi risasi kimakosa.

Mshukiwa mmoja kwa kutumia bastola yao alifanikiwa kujibu huku maafisa wa polisi wakifyatua risasi kwa ustadi mkubwa.

Bastola ya washukiwa haikuwa na risasi zaidi na ndipo maafisa hao walipofanikiwa kuwaangusha watatu hao.

Biu Nyongesa kwamba polisi walifanikiwa kupata bastola aian ya Berreta Nambari za usajili EB_190125737.

Aidha, bastola hio haikuwa na magazini.

Walipata pia vitabu mbalimbali vya shule, kitambulisho cha mwanafunzi na kitambulisho cha kitaifa cha mwanafunzi anayeaminika kuwa wa Chuo Kikuu cha Nairobi.

Miili ya wasdukiwa wote watatu ilipelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha City.

Ripoti za polisi zilionesha kuwa vitabu vilivyopatikana ni vya Bw Obunde, mwalimu mwenye umri wa miaka 25 katika Shule ya Kimataifa ya Windsor.

“Alirekodi taarifa kwamba aliibiwa begi lenye vitabu, stakabadhi zingine za kibinafsi, pesa taslimu Sh400, simu ya mkononi aina ya Techno Sparks ‘4’ yenye thamani ya Sh12,000 na pochi iliyokuwa na kadi za Bi Nyongesa akasema.

Bi Nyongesa aliongeza kuwa mwalimu wa umri wa miaka 31 katika Nairobi Leadership Academy aliibiwa tarakilishi ndogo aina ya HP yenye thamani ya Sh30,000 na simu ya rununu aina ya REDMI yenye thamani ya Sh24,000.

Mlalamishi kulingana na rekodi, zilionyesha washukiwa waliouawa walihusishwa na tukio la wizi kabla ya kuuawa na polisi.

Bi Nyongesa alisema kaunti ndogo ya Makadara iko salama na hakuna sababu ya kuwa na haja ya wananchi kuwa na wasiwasi.

“Nimeimarisha doria za polisi na kufanya kazi na DCIO wangu, Martin Korongo katika juhudi za pamoja za kukomesha uhalifu. Viwango vya uhalifu katika kaunti ndogo ni vyema siku hizi ikilinganishwa na siku za awali kutokana na mpango wa kuwasdhirikisha wanakamati wa Nyumba Kumi,” Bi Nyongesa alisema.

[email protected]