Kikosi maalumu chafanya msako wa ghafla kunasa silaha haramu
JUMAPILI iliyopita iliyokuwa tulivu kwa wakazi wa Kalemengorok, Aroo, Kaunti ya Turkana, iligeuka kuwa ya hofu baada ya maafisa wa Kikosi Maalumu cha Operesheni (SOG) kufika kwa magari ya kivita na Land Cruiser kadhaa, wakifunika nyuso zao kwa barakoa.
Utulivu wa asubuhi, ambapo watu walihudhuria ibada kanisani, kuendesha biashara kwenye soko au kufanya shughuli zao za nyumbani, ulivurugika ghafla wakati kikosi hicho maalumu kilipoanza kutembea mtaani, kikihimiza wananchi wote kuhudhuria baraza la haraka lililohutubiwa kwa dharura.
Wakazi waliokuwa wakichelewa au kubaki sokoni walidai kupigwa na kulazimishwa kuhudhuria. Walijua kuwa hii ni sehemu ya operesheni kubwa ya usalama katika mpaka wa Turkana na Pokot Magharibi iliyolenga magaidi na silaha haramu.
Katika baraza hilo, majina ya wamiliki wa silaha haramu, wakiwemo viongozi wa kisiasa, maafisa wa serikali, wanajamii wenye ushawishi, maafisa waliostaafu na hata mashujaa waliokufa, yaliyosomwa kwa sauti kubwa, yalisababisha hofu na minong’ono miongoni mwa wananchi.
Wazee wa mitaa walihitajika kuongoza kikosi kupata wahalifu, huku pia muda wa siku tatu ukitangazwa kwa wananchi kusalimisha silaha zao.
“Ilionekana wazi kuwa hii haikuwa operesheni ya kawaida ya usalama. Aliyekataa kuhudhuria baraza alipigwa na kulazimishwa kufanya hivyo. Hata wale waliokuwa wakifanya shughuli zao walilazimishwa kuhudhuria, na watu waliambiwa wana wana siku tatu kusalimisha silaha zao,” alisema Bw James Kisike, mkazi wa eneo hilo.
Viongozi wa mitaa na wakuu wa polisi walitarajiwa kutoa orodha ya wamiliki wa silaha haramu. Mchana wa siku hiyo, eneo la Kalemengorok liligeuka kuwa kituo cha hofu, na maafisa wa SOG wakikagua nyumba, kuuliza wananchi maswali na kushirikiana na viongozi wa mitaa na polisi wa akiba, huku operesheni dhidi ya majangili na wamiliki wa silaha haramu ikizidi.
Kamanda wa Polisi Kaunti ya Turkana John Tarus, alithibitisha operesheni hiyo, lakini hakutoa maelezo zaidi.
Operesheni hii ni sehemu ya “Operation Maliza Uhalifu North Rift,” juhudi ya pamoja ya Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) na Huduma ya Polisi ya Kitaifa iliyoanza Februari 2023.