• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 AM
Kiwango cha umaskini Kilifi chazua hofu

Kiwango cha umaskini Kilifi chazua hofu

NA MAUREEN ONGALA

WADAU wa elimu Kilifi wameibua wasiwasi kuhusu umaskini uliokithiri wakisema unafanya baadhi ya wanafunzi wasiojiweza waendelee kuwa nyumbani licha ya kupokea ufadhili wa masomo.

Hali hiyo mbaya ilidhihirika kutokana na maombi 2,700 yaliyopokelewa kwa ufadhili wa masomo wa mpango wa Maendeleo ya Kijamii na Kiuchumi wa shirika la Uvuvi na Ubaharia nchini (KEMFSED), ilhali ni wanafunzi 120 pekee waliolengwa.

Ufadhili huo huwa unalenga wanafunzi wa shule za sekondari, vyuo na vyuo vikuu kwa ajili ya vyeti vyao na kozi za Diploma na Elimu ya Kiufundi (TVETs).

Waziri wa Kilimo katika Kaunti ya Kilifi, Chula Mwagona, alisema awali walilenga wanafunzi 10 katika vitengo vinne katika awamu ya kwanza na ya pili lakini baadaye, Benki ya Dunia inayofadhili mpango huo ilizingatia ombi lao na kuwaruhusu kuongeza idadi ya walengwa hadi 30 katika kila kitengo.

Waziri wa Elimu katika Kaunti ya Kilifi, Felkin Kaingu, alisema wamebaini kuwa baadhi ya waliopokea ufadhili wa masomo bado wako nyumbani.

Akihutubia wanahabari wakati wa hafla ya kuwatunuku wanafunzi wenye uhitaji ufadhili huo, alisema kiwango cha mpito cha shule ya upili katika Kaunti ya Kilifi kilikuwa asilimia 85.

“Wazazi wengi Kilifi ni maskini na hata tukitoa ufadhili wa masomo, kuna wale ambao hawana uwezo wa kununua sare na kugharimia usafiri wa watoto wao, na kwa hivyo bado tuna matatizo mengi yanayoathiri sekta ya elimu,” alisema.

Mratibu wa KEMFSED Kaunti ya Kilifi, Lucy Kapombe, alisema wametoa Sh22 milioni tangu mwaka wa masomo wa 2022 hadi 2024 kwa wanafunzi 180.

Mbali na ada ya masomo, program hiyo pia inashughulikia usafiri na athari za kibinafsi kwa walengwa.

Wanafunzi wa shule za sekondari wanapata Sh10,000, na wale wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi (TVETs) na Vyuo Sh20,000.

“Suala la ukosefu wa usafiri na ununuzi liliibuka wakati wa awamu yetu ya kwanza na pili ya kutekeleza mradi na tunaweza kutoa magari yetu kuwapeleka wanafunzi shuleni,” alisema.

Bi Kapombe alisema baadhi ya wanafunzi hawawezi kumudu vitabu na kalamu na hata pesa za masurufu.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kilimo katika Bunge la Kaunti ya Kilifi, Kazungu Mbura, alisema kuna haja ya miradi ya maendeleo inayotekelezwa na mashirika ya serikali na mashirika yasiyo ya serikali kuangazia ufadhili wa elimu ili kusaidia wanafunzi mahiri na wanaotoka katika familia maskini.

 

  • Tags

You can share this post!

Kinaya Ruth Odinga akisifia utawala Gavana wa UDA

Haiti yatangaza hali ya hatari  

T L