Polisi auawa katika kisasi cha ufyatulianaji risasi na majambazi Nakuru
AFISA wa polisi alipigwa risasi na wenzake wawili kupata majeraha mabaya kutokana na kisa cha ufyatulianaji risasi na wahalifu Jumapili usiku katika eneo la Freehold, Kaunti ya Nakuru.
Polisi aliyeuawa alitambuliwa kama Josphat Ruto na alikuwa wa cheo cha konstebo. Alikuwa ameandamana na wenzake watatu wakati walipovamiwa na wezi waliojihami vikali.
Tukio hilo lilijiri walipokuwa wakipiga doria barabara ya Freehold, eneo ambalo limekuwa likishuhudia ongezeko la visa vya uhalifu wiki chache zilizopita.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Nakuru Loyford Kibaara, polisi hao bila kujua, walikabiliana na wezi hao walioaminika walikuwa wakipanga kutekeleza uhalifu.
“Kulikuwa na kisa cha ufyatulianaji risasi na Konstebo Ruto alipigwa risasi tumboni. Baadaye aliaga dunia akipokea matibabu kwenye Hospitali ya Rufaa ya Nakuru Level Five,” akasema Bw Kibaara.
Ripoti ya awali ya matibabu ilionyesha kuwa afisa huyo alikufa kutokana na kuvuja damu tumboni, maafisa wengine walioumia ni Saul Mutoro na Walter Makori.
Bw Mutoro, alipata majeraha ya kukatwa na panga kwenye mkono wake wa kulia na alitibiwa kisha akaruhusiwa kuondoka hospitalini akiwa katika hali dhabiti ki afya.
Wakati wa kisa hicho cha ufyatulianaji risasi, mmoja wa washukiwa hao wa uhalifu alipigwa risasi lakini akafanikiwa kutoroka akiwa na majeraha,
Kutokana na tukio hilo, makachero walianza operesheni kali na kuwaandama washukiwa wanne wanaoaminika kuwa sehemu ya genge hilo ambalo limekuwa likiwahangaisha wakazi wa Nakuru kwa wiki tatu sasa.
Kati ya waliokamatwa ni mwanamke mwenye umri wa miaka 45 ambaye aliwahi kutumikia kifungo gerezani na anatuhumiwa kuwa kiongozi wa genge hilo.
Bw Kibaara alisema washukiwa wanne walikamatwa wakiwa wamejificha kwenye nyumba moja ya kukodisha jijini Nakuru. Mwanamke aliyenyakwa nao alikuwa amekamilisha kifungo chake gereza la Nakuru mwezi uliopita na inaaminika amerejelea vitendo vya uhalifu.