Serikali ya Sakaja yasaka kibali cha kuzika miili 600 iliyorundikana City Mortuary
ZAIDI ya miili 600 kwa sasa inahifadhiwa katika Chumba cha Kuhifadhi Maiti cha Nairobi (zamani City Mortuary), mingi ikiwa haina watu ambao wamekuja kuidai.
Haya yanafanyika wakati ambapo chumba hicho kinaonekana kulemewa na idadi ya miili hasa ambayo hufikishwa humo baada ya kila wikendi.
Ripoti inaonyesha kuwa kila wikendi miili zaidi ya 40 hufikishwa katika chumba hicho cha kuhifadhia maiti.
“Watu hufa sana Nairobi hasa wikendi kwa sababu huwa tunapata ripoti ya zaidi ya miili 40 katika muda huo. Sijui sababu hasa nini lakini huenda vijana wanazama kwenye sherehe kisha kuendesha magari kwa kasi na pia ajali nyingi ya bodaboda hutokea,” akasema Afisa Mkuu wa anayesimamia vituo vya afya Nairobi Tom Nyakaba.
Afisa huyo alisema kuna zaidi ya miili 300 ambayo jamaa wao hawajajitokeza ilhali chumba hicho cha kuhifadhi maiti kinaweza kusitiri maiti 184 kwa wakati. Baadhi ya miili imekuwa ikihifadhiwa tangu Aprili mwaka jana.
“Ajali za barabarani kati ya Ijumaa na Jumapili ndizo zinasababisha mauti kwa wingi hasa kwa vijana. Pia tunapata miili kutokana na kitanzi, wanaouawa na umati lakini visa vya kitanzi na ajali ndivyo vingi,” akaongeza.
Ili kupisha miili mipya inayofikisha chumba hicho cha kuhifadhi maiti, kaunti imewasilisha kesi mahakani iruhusiwe kuizika miili ambayo imekwepo kwa kipindi kirefu.
“Tuna miili 294 ambayo inastahili kutupwa na tuna orodha ambayo tumewasilisha kortini kusaka amri ya kuizika. Tukipewa idhini tu, tutaizika,” akasema Bw Nyakaba.
Lakini kabla ya amri hiyo kutolewa kaunti itabidi ipambane na gharama ya juu ya kuhifadhi miili hiyo.
Miili huwa inahifadhiwa kwa miezi sita na baada ya hapo hufanyiwa upasuaji kisha notisi huchapishwa magazeti mbalimbali ambapo wenyewe wasipojitokeza kaunti huizika baada ya kupata kibali cha mahakama.