Habari za Kaunti

Shahidi adai Mackenzie alizika pia mtoto wake mchanga Shakahola

February 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MAHAKAMA imeelezwa kuwa mhubiri mwenye utata Paul Mackenzie alimzika mtoto wake mchanga katika msitu wa Shakahola.

Enos Amanya, aliyekuwa mkuu wa usalama ndani ya msitu huo, alifichua kwa mara ya kwanza kwamba hata mtoto wa Mackenzie hakunusurika katika mfungo wa kikatili uliosababisha vifo vya zaidi ya waumini 450 wa kanisa lililopigwa marufuku la Good News International (GNI).

“Mtoto wa Mackenzie mchanga ambaye bado alikuwa ananyonya alifariki. Tulimzika Galilaya,” alisema Amanya.

Galilaya ilikuwa mojawapo ya vijiji tisa vya kiutawala vilivyoanzishwa na Mackenzie ndani ya msitu wa Shakahola. Hapo ndipo walipoishi wakuu wa dhehebu waliokuwa wakisimamia vijiji vingine vinane.

Ingawa haikuwa ndani kabisa ya msitu kama makazi mengine, Galilaya ilikuwa imejitenga na maisha ya kawaida na ilikuwa makao makuu ya Mackenzie, ambako harakati zote za dhehebu hilo zilipangwa.

Amanya aliongeza kuwa binti yake, Snider Dorcas, ambaye sasa angekuwa na umri wa miaka 23, pia alizikwa Galilaya.

Hata hivyo, alisema kwamba habari zilipoenea kuwa serikali imejua kuhusu vifo hivyo na tayari ilikuwa imeanza msako, watoto wote waliokuwa wamezikwa Galilaya, akiwemo mtoto wa Mackenzie, walifukuliwa na kuzikwa upya Samaria.

Samaria ilikuwa ndani zaidi ya msitu, mbali na barabara ndogo zilizofanya Galilaya kufikika kwa urahisi.

Amanya aliiambia mahakama hatua hiyo ililenga kuficha ushahidi wa vifo vilivyotokea Galilaya, makao makuu ya Mackenzie.

“Mackenzie aliweka wazi kwamba hakutaka ushahidi wowote. Hivyo tuliamrishwa kufukua miili kutoka makaburi ya Galilaya na kuizika upya ndani kabisa ya kijiji cha Samaria,” alieleza.

Amanya mwenyewe alichimba makaburi, mbali na kuwa mlinzi wa usalama.

Aliwabeba watoto waliokuwa wamefungwa waya ili kuhakikisha wanaendelea kufunga. Watoto wake sita kati ya saba walifariki.

“Nilibeba watoto wangu wawili mabegani kwa uchungu mkubwa, nikiwaahidi kwamba nami nitawafuata kwa Yesu waliponiuliza kama nitawafuata,” alisema huku akibubujikwa na machozi.

“Mackenzie aliipatia familia yangu chakula cha mwisho kabla watoto wangu kufariki,” aliongeza.

Akiwa kizimbani kama shahidi wa upande wa mashtaka, Amanya alidai kwamba dhana ya “Jangwani” ilianzishwa kama wazo la kiroho kabla ya wafuasi kuhamia Shakahola.

“Jangwani ilielezwa kama mahali pa kiroho kwa wateule. Tulikuwa bado Nairobi wakati wazo hili lilipohubiriwa kwetu,” alisema.

Amanya alithibitisha kuwa Mackenzie aliwaambia wafuasi wake kuwa tiba ya kisasa ilikuwa uchawi na kutangaza dini kuwa ni ovu.

“Alifundisha kwamba Mungu, binadamu na serikali ni waovu,” alisema.

Serikali ilipofunga kanisa la GNI, Mackenzie alilibadilisha jina na kuliita Kanisa la Times TV.

“Alisema wakati ungefika ambapo hangeruhusiwa kuhubiri kwa sababu serikali ilikuwa imemuuliza,” Amanya alikumbuka.

Amanya alisema aliuza mali yake Nairobi kwa Sh700,000 na kuhamia na familia yake pamoja na ndugu yake Malindi, kisha kuingia msituni.

Walipoingia Shakahola, mawasiliano na watu wa nje yalikatizwa.

“Mackenzie alipiga marufuku matumizi ya simu za mkononi na kutuambia tujitenge kabisa na dunia,” alisema.

Hata hivyo, marufuku hiyo haikutumika kwa wote.

“Ni matajiri pekee walioruhusiwa kumiliki simu na hata kuwasiliana na watu wa nje au kutembelea vituo vya biashara vilivyo karibu bila vizuizi vikali,” alisema.

Matajiri waliruhusiwa kununua bidhaa, kutoa fedha na kupokea ziara za Mackenzie, mara nyingi wakimkabidhi zawadi ya fedha taslimu na mahitaji mengine.

Makazi yaligawanyika wazi kati ya wenye pesa na maskini.

“Ungeambiwa Mackenzie anatembelea familia tajiri, lakini usingemuona akifanya hivyo kwa maskini,” aliongeza.

Vizuizi viliongezeka kutoka kwenye uhuru wa kutembea hadi maombi na hata usomaji wa Biblia.

“Mackenzie aliamuru kwamba kusiwe na maombi yoyote na, ikiwezekana, Biblia zichomwe,” alisema Amanya.

Alikumbuka kisa kimoja ambapo walitumiwa walinda usalama wa maituni kuwaonya walipokuwa wakiabudu kwa sauti nyumbani kwao.

“Msitu ubaki kimya na mtu asionekane akiabudu au kuomba,” Mackenzie aliamuru.

Evans Sirya alikuwa mzee aliyesimamia vijiji vyote tisa vilivyotawanyika msituni na alikuwa kiungo kati ya Mackenzie na uongozi wa maeneo hayo.

Alisambaza maagizo kutoka kwa Mackenzie kwa viongozi wengine wa dhehebu hilo. Waliopinga amri ya Mackenzie waliadhibiwa vibaya kwa viboko.

Mlinzi mmoja wa Mackenzie aliyejulikana kama Paul aliripotiwa kupigwa na wakazi waliopinga shughuli za Mackenzie.

Badala ya kupelekwa hospitalini, Amanya alisema Mackenzie alimwambia chaguo pekee lililobaki lilikuwa “kupanda ndege kwenda mbinguni”.

“Kuenda kwa ndege” ilikuwa lugha fiche kumaanisha mfungo mkavu, bila chakula, bila maji, hadi kifo.

“Paul alifariki baadaye,” aliongeza.

Amanya amekubaliana na upande wa mashtaka na atatumikia kifungo cha miaka miwili gerezani.

Alisema Mackenzie alianzisha mfungo baada ya kubaini kuwa wangeweza kufukuzwa msituni.

Kulingana naye, zaidi ya watu 900 waliishi msituni, na zaidi ya 700 walifariki kutokana na mfungo huo.

Takwimu rasmi zinaonyesha kwamba miili 450 pekee imefukuliwa, ikionyesha kuwa wengine bado wapo katika makaburi ya kina kifupi ndani ya msitu.