Tahadhari viwango vya maji baharini vikiendelea kuongezeka kwa kasi
JAMII zinazoishi katika maeneo ya Pwani, zimepewa tahadhari kuhusu ongezeko la viwango vya maji baharini kwa kasi.
Ripoti mpya kuhusu hali ya hewa nchini inaonyesha kuwa, katika mwaka wa 2025, kulishuhudiwa ongezeko la maji baharini na mawimbi makali kuliko ilivyo kawaida.
Hali hii ilisababisha vifo, majeraha na uharibifu uliosababishwa na hali ya hewa isiyo ya kawaida katika kaunti mbalimbali za Pwani, hasa zinazopakana na Bahari Hindi.
“Kulikuwa na vipindi ambapo maji ya kila siku mwaka wa 2025 yalikuwa yanakaribia au kuzidi viwango vya juu vya kihistoria. Hii inaashiria ongezeko la kina cha maji ya Pwani,” sehemu ya ripoti hiyo iliyotolewa na Idara ya Kutabiri Hali ya Hewa nchini ikaeleza.
Maelezo hayo yanatarajiwa kuwa muhimu katika upangaji na maisha ya kila siku, hasa kwa jamii na biashara zinazotegemea bahari kwa riziki, mbali na idara za utawala zinazotakikana kukabili majanga au kuyaepusha.
Ripoti hiyo imetoa ilani kuwa, ijapokuwa viwango vya juu vya maji ni muhimu kwa meli kutia au kung’oa nanga bandarini, “vinaweza kuongeza hatari vinapochanganyika na mawimbi, mikondo ya maji au dhoruba za baharini.”
Ingawa mabadiliko haya huenda yasionekane makubwa mara moja, athari zake za kudumu zishaanza kubadilisha maisha ya watu, kama vile eneo la Kipini, Tana River ambako kuna kijiji kilichofunikwa na bahari, na sehemu za Kwale ambako pia hali kama hiyo imeanza kushuhudiwa.
Hii hutokana na jinsi ongezeko la kina cha bahari husababisha maji kufika mbali zaidi ndani ya nchi kavu, na kuongeza pia hatari ya mafuriko katika maeneo ya chini.
“Kuongezeka mara kwa mara au kwa muda mrefu kwa viwango vya maji baharini kunaweza kusababisha mmomonyoko wa ufukwe, uharibifu wa miundomsingi ya pwani, na mafuriko katika nyanda za chini,” ripoti inaeleza.
Utalii, ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa Pwani, nao pia uko hatarini.
Kadri mmomonyoko wa ardhi unavyoongezeka na maji kusogea ndani ya nchi kavu, hoteli na sehemu za burudani zilizo kando ya ufuo huanza kuathiriwa.
Kwa wavuvi wadogo, hatari ni ya moja kwa moja zaidi kwani bahari inapochafuka, huweka maisha yao hatarini.
“Kuongezeka kwa mawimbi ya bahari na viwango vya maji kunaweza kuathiri wavuvi kupata maeneo ya kutia nanga, muda wa kuondoka na kurejea nchi kavu, na usalama wa shughuli za karibu na ufukwe,” ripoti ikasema.
Mifumo ya ikolojia ya pwani, ambayo kwa kawaida hutoa kinga ya asili kwa mazingira, nayo pia huathirika.
Mikoko na nyasi baharini hutegemea uwiano maalumu wa maji na mchanga. Ingawa mafuriko ya mara kwa mara yanaweza kusaidia, ongezeko la maji huvuruga mifumo hii.