Ugawaji misaada bila mpangilio umeongeza ombaomba mitaani, Gavana Nassir alalama
GAVANA Abdulswamad Nassir ametaka kuwe na mwongozo maalumu kuhusu utoaji misaada kwa jamii zisizojiweza, ili kupunguza idadi ya familia zinazorandaranda mitaani jijini humo.
Kulingana naye, mazoea ya wakazi na makampuni kupeana misaada kama vile vyakula yamechangia ongezeko la ombaomba katikati ya jiji, hali ambayo inahofiwa kutatiza pia usalama.
“Tumefika hapa kwa sababu ya kugawa vyakula vya msaada bila mpangilio. Ninawaomba tudhibiti shughuli za misaada katikati mwa jiji. Utoaji misaada usiodhibitiwa unawavutia watu wasiojiweza kuingia katikati ya jiji,” alisema.
Bw Nassir alikiri kuna changamoto ya familia za mitaani ambao wamevamia mji huo na kufanya barabara zingine kuwa makao yao.
Hata hivyo, aliwahakikishia wadau wa utalii na wakazi kwamba serikali yake itakabiliana na tatizo hilo.
Baadhi ya wakazi walisema kuwa wamelazimika kuajiri walinzi binafsi kulinda milango yao ili kuzuia familia za mitaani kuingia kwenye makazi yao, wakieleza hofu ya usalama.
Maeneo sugu ni kama vile Makadara, Bustani ya Mama Ngina, nje ya kituo cha polisi cha Urban na Kizingo.
Akizungumza baada ya kukutana na wakazi wa Mji wa Kale pamoja na diwani wa wadi hiyo Bw Abdirahman Hussein, Gavana alieleza hatua ambazo serikali yake imechukua ikiwemo kushirikiana na maafisa wa usalama na kutia mbaroni mamia ya familia hizo tangu Januari.
“Kuanzia Januari hadi Machi 22, 2026, tumekamata watu 428. Tangu Machi 23, 2026 hadi sasa, watu wengine 271 wamekamatwa, huku 123 tayari wakishtakiwa mahakamani,” alisema Bw Nassir.
Gavana Nassir alisema kuwa idadi kubwa ya waliokamatwa ni watoto wadogo.