Habari za Kaunti

Ukipata tiketi ya urais, nitakuunga mkono, Arati aambia Matiang’i

Na  WYCLIFFE NYABERI March 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Gavana wa Kisii Simba Arati amedokeza kuwa yuko tayari kumuunga mkono naibu kiongozi wa chama cha Jubilee Dkt Fred Matiang’i katika azma yake ya urais ila kwa sharti moja; ikiwa mrengo wa upinzani utamteua Waziri huyo wa zamani wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiangi kama mwaniaji wao wa urais.

Mbunge huyo wa zamani wa Dagoretti Kaskazini, aliongeza kuwa iwapo hilo litatimia, basi atatumia rasilimali yake ili kumpigia debe Dkt Matiang’i achaguliwe rais wa sita wa Jamhuri ya Kenya.

“Nataka kuwaambia wenzetu wanaozunguka na ndugu yetu kuwa, nyinyi mfanye yeye awe mwaniaji wenu wa urais. Mtaniona nikiuza hata gari langu la Range Rover ili kumpigia debe kote nchini,” Bw Arati alisema Jumatano ugani Gusii, wakati za hafla ya uzinduzi wa matingatinga ambayo serikali yake imenunua ili kusaidia katika ukarabati wa barabara. inasemekana kuwa matingatinga hayo 32, yalimgharimu mlipa ushuru kima cha zaidi ya Sh 1.4 bilioni.

Licha ya kutoka katika jamii moja na Dkt Matiang’i, Bw Arati hajakuwa akiichangamkia azma ya Dkt Fred Matiang’i ya kuwania urais na badala yake, amekuwa akiirai jamii kumuunga mkono rais William Ruto kwa muhula wake wa pili, akijitetea kuwa hiyo ndiyo njia ya pekee ambapo wakazi wa Kisii wanaweza kupata maendeleo.

Katika hafla nyingi ambazo anampigia Dkt Ruto debe, Bw Arati amekuwa akimfananisha rais na ng’ombe wa maziwa.

Gavana wa Kisii Simba Arati ahudhuria umati wa watu ugani Gusii mnamo Machi 18,2026/PICHA/WYCLIFFE NYABERI

“Watu wangu, si mkubali tumkamue huyu ng’ombe kwanza na ukifika muda mzuri tutaamua tutakapoenda? Unaweza kumkamua ng’ombe kweli ilhali unamcharaza viboko?” Arati aliuliza umati uliojaza uga huo wa Gusii ili kushuhudia matingatinga hayo.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Waziri wa Elimu Julius Migos Ogamba pamoja na wabunge wengine kutoka eneo pana la Gusii wanaoshabikia serikali jumuishi.

Wakiongozwa na Bw Ogamba, wabunge hao walikenua meno yao dhidi ya aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua kwa matamshi yake wakati alipozuru eneo la Gusii na viongozi wengine wa upinzani.

Viongozi hao walimtaja Bw Gachagua kama mkabila na anayepania kuizamisha jamii ya Abagusii.

“Hatutakubali mtu yeyote kuwapotosha watu wetu kwa semi za chuki na ukabila zinazotishia umoja wetu. Tutazidi kuwalinda watu wetu na kumuunga mkono rais wa sasa William Ruto,” Waziri Ogamba alisema.

Mbunge wa Mugirango Kusini na Kinara wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Silvanus Osoro, aliwaeleza viongozi hao wa upinzani kujiandaa kwa dhihaka zingine ambazo watakuwa wanaelekezewa na mrengo wa serikali.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo ni wabunge Japheth Nyakundi (Kitutu Chache Kaskazini), Alfah Miruka (Bomachoge Chache), Steve Mogaka (Mugirango Magharibi), Daniel Manduku (Nyaribari Masaba) Zaheer Jhanda (Nyaribari Chache), mbunge mteule Irene Mayaka miongoni mwa wengine.