Viongozi wasihi misaada imiminike kwa Waislamu maeneo kame msimu huu wa mfungo
BAADHI ya viongozi wa kidini na waumini wa Kiislamu wametaka jamii zinazoishi katika maeneo yanayokumbwa na ukame wapewe misaada ya dharura wakati wanapoanza mfungo wa mwezi wa Ramadhan.
Ramadhani ya mwaka huu, inayotarajiwa kuanza leo (Februari 18) au kesho, inaadhimishwa wakati ambapo sehemu kadhaa za nchi zinakabiliwa na ukame.
Baadhi ya kaunti zilizoathirika na ukame ni Mandera, Turkana, Wajir, Garissa, Marsabit, Isiolo, Kajiado, Kilifi, Kwale, Tana River na maeneo ya Lamu.
Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Waislamu nchini (SUPKEM) tawi la Lamu Mohamed Abdulkadir, alisema kufunga wakati kuna uhaba mkubwa wa maji mara nyingi huathiri afya, kusababisha kizunguzungu na hata mtu kupoteza fahamu, hasa hali hiyo inapochanganyika na joto kali linalosababishwa na ukame.
Vilevile, Bw Abdulkadir alisema hali ya ukame hufanya wengi kukosa kuhudhuria ibada katika misikiti mingi.
“Badala ya waumini kuzingatia ibada ya kufunga na swala za pamoja, wanalazimika kutanguliza suala la kujiokoa kwa sababu ya uhaba wa maji unaohitajika kwa udhu katika misikiti hiyo. Ni kipindi ambacho waumini katika maeneo kama Basuba hulazimika kusafiri mbali kutafuta maji na hatimaye hukosa mahubiri na swala misikitini,” alisema Bw Abdulkadir.
Bw Mahmoud Ahmed, kiongozi wa kidini wa Kiislamu, alisisitiza kuwa wakati wa ukame huwa na joto kali, jambo linaloongeza zaidi hatari ya upungufu wa maji mwilini.
“Ramadhan ni kipindi ambacho sisi Waislamu tunapaswa kufunga. Hakuna kula wala kunywa maji kwa angalau saa 14. Hiyo inamaanisha hakuna chakula wala maji kuanzia alfajiri hadi machweo. Kukosa maji safi au hata mahitaji ya msingi kunafanya kufunga kuwa hatari, na huongeza hatari ya kizunguzungu, matatizo ya figo na utapiamlo,” alisema Bw Ahmed.
Bi Maryam Abatika wa Kijiji cha Basuba katika Msitu wa Boni, aliomba serikali ya kaunti na serikali ya kitaifa kuzingatia kusambaza chakula cha msaada na maji.
Kwa sasa, eneo kubwa la Basuba linakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula na maji, hali ambayo Bi Abatika anahofia inaweza kusababisha wengi kushindwa kuzingatia Ramadhan.
“Hatuna maji wala chakula cha kupika wakati wa iftar au suhoor. Tutafanyaje katika hali hii? Hiki ni kipindi ambacho maji yanahitajika sana kwa kila jambo linalohusiana na Ramadhan, lakini hayapo. Kuna haja ya hatua za haraka kuchukuliwa,” alisema Bi Abatika.
Hata hivyo, viongozi na waumini wengine walisema ukame wakati wa Ramadhan ni kama jaribio la subira na imani, jambo linaloweza kuongeza dua, ibada na mshikamano wa kijamii.
Walieleza pia kuwa, mafundisho ya Kiislamu yako wazi kwamba wale wanaoweza kupata madhara wameruhusiwa kutofunga au kuvunja saumu na kuilipa baadaye au kutoa fidia, kulingana na hali zao.