Vyama vidogo vyalia ODM inavimalizia ushawishi katika Kenya Kwanza
VYAMA vidogo ndani ya Kenya Kwanza vimeanza kulalamika kuwa, ODM inaviengua baada ya kuanzishwa kwa mazungumzo kuhusu muafaka na UDA kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Uhasama kati ya vyama vikubwa na vidogo ulichipuka hivi majuzi Naibu Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Owen Baya, mwandani wa Rais Ruto, alisema PAA inayoongozwa na Spika wa Bunge la Seneti Amason Kingi haina ushawishi.
Bw Baya tayari amesema kuwa anaunga mkono Gavana Gideon Mungáro kwa muhula wa pili mnamo 2027.
Mbunge huyo wa Kilifi Kaskazini amesema PAA haiwezi kulinganishwa na ODM ambayo ipo katika ushirikiano na Rais William Ruto na ina sura ya kitaifa.
“Ningependa kusema hii hadharani na kwa umma kuwa hapa Kilifi kuna vyama viwili ambavyo ni UDA na ODM. Hivyo ndivyo vyama ambavyo vina mizizi hapa,” akasema Bw Baya.
Kando na PAA vyama vingine ambavyo vina muafaka na UDA ni ANC na Maendeleo Chap Chap (MCC).