Habari za Kaunti

Wakazi wataka maisha bora baada ya ujangili kuzimwa mpakani

Na SAMMY LUTTA August 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KWA zaidi ya miongo mitatu, wakazi wa Lorogon, mpakani mwa Turkana na West Pokot, wameishi kwa hofu ya majangili wenye silaha.

Lakini sasa bunduki zimetulia kwa kiasi kikubwa kufuatia operesheni ya serikali ya kuwapokonya silaha wahalifu hao, na wakazi wanataka amani hiyo iwaletee ajira, maji, umeme na maisha bora.

Lorogon iko kati ya Mto Turkwel na vilima vyenye mabonde magumu kufikika, ambayo kwa miaka mingi yamekuwa maficho ya majangili.

Hapo, maisha yalitawaliwa na milio ya risasi huku watoto, wanawake na wazee wakiathirika. Baadhi ya familia zimebaki na makaburi ya wapendwa wao waliouawa katika ghasia hizo.

Ukosefu wa usalama pia uliathiri uchumi. Wakulima walishindwa kufikia mashamba yao, huku mifugo, ambayo ndiyo tegemeo la familia nyingi, ikiibwa mara kwa mara.

Hata safari ya kutafuta maji iligeuka kuwa hatari.

Bi Leah Natuk alisema wakazi walikuwa katika hatari ya kushambuliwa wakati wowote makundi hasimu yalipofanya mashambulizi ya kulipiza kisasi.

Alikumbuka tukio la mwaka 2013 ambapo majangili walizingira kijiji hicho kwa siku tano baada ya kuziba barabara kutoka Kainuk kupitia Sarmach na Turkwel.

Walikata miti mikubwa, kuchimba mashimo na kuweka mawe barabarani kuzuia magari kuingia au kutoka.

“Majangili walitaka kutulazimisha kuondoka katika kijiji cha mababu zetu kwa sababu tulisisitiza kuwa kiutawala na kisiasa tunahusishwa na Kaunti ya Turkana,” alisema.

Sasa usalama unaporejea, wakazi wameanza kuangalia zaidi ya kuishi kwa hofu.

Katika mkutano wa wadau uliofanyika Shule ya Msingi ya Lorogon, walishukuru serikali kwa kurejesha usalama na kusema wanaweza kusafiri hadi Kainuk bila kusindikizwa na polisi.

Naye Bi Esther Piarai, alitaka idadi ya Polisi wa Akiba iongezwe, akisema kijiji hicho kina askari watatu pekee.

Pia alitaka wenyeji wapewe ajira katika ujenzi wa bomba la maji linalotarajiwa kujengwa na Jeshi la Ulinzi la Kenya.

“Tunaomba tupewe nafasi ya haki katika ajira zitakazopatikana wakati wa ujenzi wa bomba la maji,” alisema.

Wakazi pia wanataka mfumo wa zamani wa maji urejeshwe na kijiji kiunganishwe na umeme.

Mkazi Peter Lochuge alisema hali hiyo ni ya kushangaza kwa kuwa Lorogon iko takriban kilomita mbili kutoka kituo cha kuzalisha umeme cha Turkwel chenye uwezo wa kutoa megawati 106.

“Tuko kilomita mbili tu kutoka kituo hicho lakini tumekosa umeme kwa zaidi ya miaka 30,” alisema.

Wakazi pia wanatarajia kunufaika na mradi wa unyunyuzaji wa Lower Turkwel wa thamani ya Sh1.8 bilioni.

Mradi huo utahusisha ekari 1,000 na kutumia maji kutoka Bwawa la Turkwel Gorge.

Waziri wa EAC ASAL na Maendeleo ya Kikanda Beatrice Askul alisema mradi huo utasaidia kuongeza uzalishaji wa chakula, kuunda ajira na kuimarisha amani.

Gavana wa Turkana Jeremiah Lomorukai alisema ushirikiano wa jamii ni muhimu ili mradi huo ufanikiwe.

Alitaka serikali kuharakisha kupokonya wakazi silaha haramu, akisema ni kikwazo kikubwa kwa maendeleo na utulivu wa eneo hilo.