Habari za Kaunti

Wakulima wafunzwa kuepuka mbegu feki

Na WYCLIFFE NYABERI  February 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Wakulima katika eneo la Nyanza wamepokea hamasisho kuhusu namna ya kukabiliana na pembejeo feki.

Hatua hii inalenga kuwaepusha na hasara zinazotokana na ununuzi wa bidhaa ghushi msimu wa upanzi ukianza kufuatia mvua inayonyesha katika maeneo mengi ya nchu.

Hamasisho hilo lililoandaliwa mjini Kisii wiki hii, liliwaleta pamoja wakulima kutoka kaunti za Narok, Migori, Homabay na Nyamira.

Hamasisho hilo liliongozwa na mashirika mbali mbali yanayoongoza vita dhidi ya pembejeo feki kama vile Bayer East Africa, kampuni ya mbegu ya Dekalab na mengine.

Afisa Mkuu Mtendaji wa Bayer East Africa John Kanyingi alidokeza kuwa Kenya ni miongoni mwa mataifa ambayo kero la kughushiwa kwa bidhaa kama vile pembejeo lilikuwa limekithiri.

Bw Kanyingi aliwataka wakulima  kununua mbegu na pembejeo zingine kutoka kwa maduka na maajenti ambao wameidhinishwa na asasi muhimu za serikali kama vile Shirika la Kephis, ambalo linahusika na afya ya mimea.”Wakulima wanafaa wawe macho wasiuziwe pembejeo feki msimu huu. Ndiyo maana tumekuja kuwaeleza wakulima kuhusu mpango huo,” Bw Kanyingi alisema.

Alionya kuwa mbegu ghushi ni tishio kubwa la kiuchumi, kwani wakulima mara nyingi hutumia pesa zao walizochuma kwa bidii kwa mbegu ambazo zinashindwa kutoa mavuno yanayotarajiwa.

“Mkulima anaponunua mbegu ambayo haifanyi kazi, inaleta tija ndogo na hasara ya kifedha. Mbegu halisi zilizoidhinishwa huhakikisha viwango vya juu vya kuota na utendakazi bora,” Kanyingi aliongeza.

Alibainisha kuwa siku za nyuma wakulima walikuwa wakipanda hadi mbegu nne katika shimo moja kwa matumaini kwamba angalau moja ingeota.

Kufuatia kuboreshwa kwa mbegu zonazouzwa na mashirika halali, Bw Kanyingi alisema mbegu zilizoidhinishwa sasa zinatoa karibu asilimia 100 ya mazao zinapopandwa kwa usahihi.