Habari za Kaunti

Wawili mahakamani kwa kujaribu kumtilia sumu mgonjwa hospitalini

Na WYCLIFFE NYABERI June 5th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WANAUME wawili wanaodaiwa kujaribu kumwekea mgonjwa sumu katika hospitali ya kibinafsi mjini Kisii watasalia rumande kwa siku 14 kabla ya kufunguliwa mashtaka mahakamani.

Wawili hao — Bendyer Gwako Onyango na Samweal Bundi Ndege Jumatano asubuhi walifikishwa katika Mahakama ya Kisii lakini hawakujibu mashtaka kwa kuwa polisi waliomba muda zaidi kukamilisha uchunguzi wao.

Ombi la upande wa mashtaka la kuwataka wawili hao wazuiliwe kwa wiki mbili lilikubaliwa na Hakimu Mkuu Mwandamizi Joshua Nyariki.

Wawili hao walimwendea mhudumu mmoja wa matibabu katika kituo hicho kilicho kando ya Barabara Kuu ya Kisii-Migori na kujaribu kumpa hongo ya Sh10,000 ili kumdunga sindano ya kuua mgonjwa mzee aliyekuwa chini ya uangalizi wake.

Mhudumu hyo aliyekatika mpango wa kutafuta ujuzi (intern), hata hivyo, alikataa ofa hiyo na kuwafahamisha mara moja wasimamizi wa hospitali ambao waliwaarifu polisi.

 Polisi waliitikia dharura hiyo na kufululiza moja kwa moja hapi hospitalini humo ambapo waliwatia wanaume hao mbaroni.

Alipofahamishwa kuhusu jaribio hilo la kumuua, mlengwa wa njama hiyo, mzee wa miaka 82, alisali.

“Bwana nakushukuru kwa siku ya leo, adui zangu walikuja kwa siri ili kuniangamiza lakini walichopanga gizani ulikiweka wazi. Nilijilaza kitandani bila kujua nia yao lakini bado ulinikinga na kuwafichua, kwa hilo nakushukuru,” mzee huyo mgonjwa alisikika akiomba.

Mgonjwa huyo pia alitoa shukrani za dhati kwa wafanyikazi wa hospitali hiyo na maafisa wa polisi kwa kuzuia jaribio hilo la mauaji.

Juhudi za Taifa Leo kupata maelezo zaidi kutoka kwa wakuu wa polisi katika kaunti hazikufua dafu.

Kamanda wa Polisi wa Kisii Ronald Kirui alituelekeza tuzungumze na kamanda wa kaunti ndogo ya Kitutu ya Kati Bw Kazungu Charo.

Bw Charo hata hivyo alilenga simu zetu, na badala yake akaandika arafa kuwa atapiga simu baadaye lakini hakufanya hivyo kufikia kuchapishwa kwa habari hii.

Naye kamishina wa kaunti ya Kisii Joseph Kibet alisema hakuwa na habari zozote kuhusu suala hilo.

“Tafadhali zungumza na kamanda wa kaunti. Sina habari,” Bw Kibet aliambia Taifa Leo kwa njia ya simu.