Wetang’ula ahimiza wakazi wa Pwani kukubaliana wawaniaji kuepuka ushindani mbaya
SPIKA wa Bunge la Kitaifa, Bw Moses Wetang’ula amewashauri wakazi wa maeneo ya Pwani na Kenya kwa jumla ambako makabila mbalimbali huishi kukumbatia demokrasia ya majadiliano na maridhiano kuepuka mizozo wakati wa Uchaguzi Mkuu ujao wa 2027.
Demorasia ya majadiliano au maridhiano ni mfumo wa kisiasa ambapo jamii au koo zinakaa pamoja na kukubaliana ni nani atashikilia wadhifa gani kabla ya kura kupigwa.
Ikumbukwe kuwa kaunti kama vile Lamu ina makaliba karibu yote ya Kenya yanayoishi eneo hilo.
Makabila mawili, ikiwemo wenyeji ambao ni Waswahili wa asili ya jamii ya Wabajuni na Wakikuyu ndiyo yenye idadi kubwa ya watu wanaoishi Lamu.
Akizungumza Jumapili wakati wa hafla ya kutoa zawadi kwa wanafunzi wa Shule za Sekondari ya Wasichana ya Pate huko Lamu Mashariki baada ya kufanya vyema katika KCSE wa mwaka 2025, Bw Wetang’ula alisisitiza haja ya jamii mbalimbali zinazoishi Lamu kuja pamoja na kuafikiana endapo jamii mwenyeji atawania kiti gani ifikapo Uchaguzi Mkuu wa 2027 ilhali viti vingine vikiachwa wazi kung’ang’aniwa na kila jamii ipatikanayo Lamu.
“Ni vyema kuzingatia demokrasia ya maridhiano tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu wa 2027. Najua hapa Lamu tunaishi makabila mengi. Ila kuja pamoja na kuridhiana ni kiti gani kiachiwe jamii mwenyeji na ni gani tukipiganie sote litakuwa suala mwafaka litakalopunguza migogoro ya kikabila na kuhakikisha usawa katika kugawana mamlaka,” akasema Bw Wetang’ula.
Alisisitiza kuwa licha ya Kenya kuwa nchi ya demokrasia, kumaanisha utambuzi wa ‘wengi wape,’ si jambo la busara kushikilia msimamo huo na kisha kuacha vyeo vote kushikiliwa na kabila moja lenye idadi kubwa kwenye eneo husika.
“Tusijikite tu kwenye msimamo wa wengi wape. Ikiwa kabila moja ndilo litakalotwaa kila kitu, huenda demokrasia hapo ikaleta matatizo. Na ndiyo sababu ninawashauri leo hii nyinyi wakazi wa Lamu kukumbatia demokrasia ya maridhiano na makubaliano ili tuishi sote kwa Amani,” akasema Bw Wetang’ula.
Jumatatu, kauli ya Spika Wetang’ula ilipokelewa na wakazi na wachanganuzi wa kisiasa kwa hisia tofauti.
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Manispaa ya Lamu, Bw Omar Famau na Diwani wa Zamani wa Mpeketoni, Bw Francis Njeru Chege, wote waliunga mkono mfumo huo mia fil mia.
“Hilo ni suala zuri na lenye kuzingatia hekima ya hali ya juu. Tunaunga mkondo Wetang’ula kwani kupitia mfumo huo, tutapunguza ule ushindani mkali wa mtu binafsi kwani viongozi watateuliwa au kuchaguliwa kupitia makubaliano ya pamoja,” akasema Bw Famau.
Bw Chege alishikilia kuwa demokrasia ya maridhiano mara nyingi huleta amani, kupunguza ghasia za uchaguzi, na kuhakikisha jamii ndogo pia hazitengwi.
Bi Mercy Muchiri kwa upande wake aliuosoa mfumo huo akisema unazuia watu kujieleza wenyewe binafsi.
“Kuna hatari ya jinsia ya kike, hasa Lamu ambako kumetawaliwa na taasubi ya kiume kubaguliwa kiuongozi. Hili litasababisha uongozi mbaya kwa sababu viongozi wanawajibika kwa wazee wa jamii badala ya wapiga kura,” akasema Bi Muchiri.