Afueni kwa wafanyakazi 7,000 wastaafu serikali ikianza mchakato wa kuwalipa
WIZARA ya Fedha imeanza mchakato wa kulipa pensheni kwa takriban wastaafu 7,000, wakiwemo walimu, hatua inayotarajiwa kuwaletea nafuu baada ya miezi kadhaa ya kuteseka tangu waondoke katika utumishi wa umma bila kupokea malipo yao.
Kucheleweshwa kwa malipo hayo kulitokana na mvutano kati ya Idara ya Pensheni katika Wizara na Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA) kuhusu utekelezaji wa sheria iliyoanza Desemba 2024 inayotoa msamaha wa kodi kwa marupurupu ya pensheni.
Huku wizara ikitaka wastaafu wote ambao marupurupu yao hayakuwa yameshughulikiwa wanufaike na msamaha huo, KRA imesisitiza kuwa unapaswa kutumika tu kwa malipo yanayoanza baada ya Desemba 27, 2024, tarehe ambayo sheria hiyo ilianza kufanya kazi.
“Ili kuzuia mateso zaidi kwa wastaafu 7,000 walioathirika, Idara ya Pensheni imeamua kuanza mara moja kushughulikia malipo hayo kwa kuzingatia mfumo wa kodi uliokuwepo kabla ya marekebisho,” alisema Waziri wa Fedha John Mbadi.
Hii ina maana kuwa wastaafu ambao malipo yao hayakuwa yametayarishwa kufikia wakati msamaha ulipoanza, watatozwa kodi kwa mujibu wa sheria ya awali.
Wakati huo huo, Wizara imeomba ushauri wa kisheria kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhusu iwapo msamaha huo unapaswa kutumika kwa kesi za mpito.
Iwapo ushauri huo utaelekeza kuwa walipaswa kusamehewa kodi, utaratibu utawekwa wa kurejesha fedha zilizokatwa.
Mbadi alifafanua kuwa maafisa wote wa umma wanaostaafu kuanzia Desemba 27, 2024 wameondolewa kabisa katika ulipaji wa kodi kwa pensheni ya kila mwezi.
Sheria hiyo inalenga kuongeza mapato mikononi mwa wastaafu na kuwasaidia kukabiliana na gharama ya maisha.
Hata hivyo, huku wizara na KRA zikiendelea na mashauriano, maelfu ya faili za pensheni zilikwama katika Jengo la Bima House.
Baadhi ya wastaafu wamesema walikuwa wakitembelea ofisi hizo mara kwa mara bila kupata majibu ya kuridhisha.
Mwalimu mstaafu David Thaguambi, aliyeondoka kazini Julai 1, 2024, alisema ameishi kwa shida kutokana na mkanganyiko huo.
Katibu Mkuu wa chama cha wastaafu, Kepha Mshambala, alikaribisha uamuzi huo, akisema umechelewa mno, na kwamba kucheleweshwa kwa pensheni kumewaweka wazee katika umaskini wakati wanastahili kuishi kwa heshima.