Habari za Kitaifa

Amerika yaiwekea Rwanda vikwazo kwa kuwaunga mkono waasi wa M23

Na MASHIRIKA March 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SERIKALI ya Amerika imetangaza vikwazo dhidi ya Jeshi la Rwanda na maafisa wake wanne kwa tuhuma za kuliunga mkono kundi la M23 linalohusishwa na mashambulizi Mashariki mwa Congo.

Tangazo hilo lilitolewa jana jioni na Wizara ya Fedha ya Amerika ambayo imedai kwamba bila msaada wa serikali na jeshi la Rwanda, kundi la M23 lisingeweza kufanya mashambulizi nchini Congo.

Kwa miaka mingi sasa inaaminika kuwa Rwanda ndiye mfadhili mkuu wa kundi la M23.

Miongoni mwa waliowekewa vikwazo ni Mkuu wa Jeshi la Rwanda, Jenerali Mubarakh Muganga, Mnadhimu Mkuu wa Jeshi, Vincent Nyakarundi na makamanda wengine wawili wa ngazi ya juu.

Utawala wa Rais Donald Trump umekasirishwa na kuendelea kwa mashambulizi ya kundi la M23 licha ya kutiwa saini kwa makubaliano ya amani kati ya Marais Felix Tshisekedi wa Congo na Paul Kagame wa Rwanda mjini Washington Desemba mwaka jana.

Rais wa Rwanda Paul Kagame ameshutumu hatua hiyo ya Amerika akisema kuwa haifai hata kidogo.