Habari za Kitaifa

Amerika yataka uchunguzi wa kina kuhusu kifo cha Ojwang

Na BENSON MATHEKA June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

AMERIKA imejiunga na Wakenya kulaani kifo cha mwalimu na mwanablogu, Albert Ojwang’, aliyefariki katika hali tata akiwa mikononi mwa polisi.

Kupitia taarifa fupi iliyotolewa Jumatano, ubalozi wa Amerika jijini Nairobi ulisema unaunga mkono wito wa uwajibikaji na uwazi katika uchunguzi unaoendelea.

“Kwa kuzingatia wasiwasi kuhusu mazingira ya kifo cha Ojwang’, Ubalozi unaunga mkono wito kutoka kwa serikali, wabunge, na wananchi wa Kenya wa kutaka uwajibikaji kupitia uchunguzi ulio wazi,” ilisema taarifa hiyo.

Ubalozi pia umetaka Mamlaka Huru ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) kupewa uwezo kamili wa kukamilisha uchunguzi wake bila vizingiti.

“Ubalozi unahimiza Mamlaka Huru ya  Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) kuendesha uchunguzi wake kwa haraka na kwa kina. Tunaitaka pia serikali ya Kenya kuhakikisha IPOA inapata usaidizi na taarifa inazohitaji kutekeleza majukumu yake.”

Wakati huo huo ubalozi huo pia ulituma rambirambi kwa familia na wapendwa wa marehemu Ojwang’.

“Ubalozi wa Amerika nchini Kenya unatuma rambi rambi kwa familia na wapendwa wa Albert Ojwang’ katika kipindi hiki cha majonzi.”

Kauli  ya Amerika ilijiri saa chache baada ya Rais William Ruto kuvunja kimya chake kuhusu tukio hilo, hatua inayotafsiriwa kama kuonyesha msimamo rasmi wa serikali kufuatia wito wa uwajibikaji.

Kupitia taarifa, Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed, alisema Rais Ruto aliagiza Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) kushirikiana kikamilifu na IPOA ili kufanikisha uchunguzi kuhusu mazingira yaliyosababisha kifo cha Ojwang’.

“Kwa hivyo naiagiza Huduma ya Taifa ya Polisi kushirikiana kikamilifu na IPOA na kuchukua hatua zote zinazohitajika kuhakikisha uchunguzi wa haraka, wa wazi, na wa kuaminika kuhusu kifo cha Ojwang’,” alisema Rais Ruto.