Habari za Kitaifa

Bango la kumsaka gaidi Banati aliyewekewa zawadi ya Sh1.3bn na Amerika latikisa utalii Lamu

Na KALUME KAZUNGU June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WASHIKADAU wa sekta ya utalii katika Kaunti ya Lamu, wamelalamika kuhusu bango linalotangaza kusakwa kwa mshukiwa sugu wa ugaidi, Abdullahi Banati, lililoezekwa Mokowe.

Wadau hao walieleza hofu kuwa, bango hilo linawatia wasiwasi wageni wanaotaka kuzuru Lamu kwani wanaona ni kama hakuna usalama.

Bango hilo lililoandikwa kwa lugha ya Kiswahili na Kisomali, linawarai wananchi wenye taarifa zozote kumhusu Banati waarifu polisi ili akamatwe.

Serikali ya Amerika ilikuwa imetenga zawadi ya Sh1.3 bilioni kwa yeyote atakayesaidia kumkamata mshukiwa huyo sugu wa ugaidi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii Lamu (LTA), Bi Fridah Njeri, aliishinikiza serikali kupitia wizara husika kuliondoa bango hilo.

Kulingana naye, sekta hiyo kwa sasa iko chini, ambapo inatimiza kati ya asilimia 35 hadi 40 pekee na hivyo basi hatua yoyote ya kutia hofu wageni inaleta hasara.

“Nimepokea malalamishi kutoka kwa wamiliki wa hoteli, hasa maeneo ya Mokowe kwamba wageni karibu 50 waliokuwa wamepanga kukodisha vyumba pale, walikatiza mipango yao punde walipofika na kuona tangazo la gaidi huyo likiwa limetundikwa kwenye bango kubwa. Hatutaki wageni wetu kufikiria kuwa sisi tumemficha huyo gaidi au Lamu si salama. Ni vyema bango liondolewe kuiokoa sekta hii muhimu,” akasema Bi Njeri.

Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii na Maendeleo kwenye manispaa ya Lamu, Bw Abdallah Fadhil, alisema hajafurahishwa na hatua hiyo.

Picha za bango la gaidi wa kimataifa anayetafutwa, Abdullahi Banati lililotundikwa eneo la Mokowe Jeti, Lamu. Bango hilo limewachukiza wadau wa utalii wakiwashinikiza wahusika kuliondoa wakidai linafurusha watalii.
Picha|Kalume Kazungu

Alieleza kuwa, eneo hilo tayari limekuwa na matatizo ya muda mrefu kuhusiana na utovu wa usalama unaochangiwa na al-Shabaab ila utulivu umeshuhudiwa kwa muda mrefu sasa.

“Ilitosha wao wamtangaze gaidi kwenye redio, magazeti, televisheni na hata mitandaoni. Kutuwekea bango hilo Lamu kunaleta uoga kwa wengi kama kwamba Lamu ina uhusiano na gaidi. Bango liondolewe mara moja,” akasema Bw Fadhil.

Alieleza masikitiko yake kwamba tangu Januari mwaka huu, sekta ya utalii imekuwa ikifanya vibaya.

“Hoteli na gesti nyingi zimekuwa zikipokea idadi ndogo ya wageni wanaokodi vyumba. Utapata wageni hawafiki hata asilimia 20 ilhali hoteli na gesti nyingine zikikosa kupata chochote. Lazima tuitunze hii sekta yetu ya utalii kwa kuhakikisha ni matangazo mazuri pekee yanapeperushwa. Hili la gaidi limeudhi wengi,” akasema Bw Fadhil.

Wadau hao wameamua kutuma wajumbe kukutana na Waziri wa Usalama, Bw Kipchumba Murkomen na mwenzake wa Utalii, Bi Rebecca Miano, ili kujadiliana kuhusu hatima ya bango hilo.

Hata hivyo, Kamishna wa Kaunti ya Lamu, Bw Wesley Koech, alisema hajafahamu kuwepo kwa bango hilo Mokowe.
Bw Koech aliahidi kufuatilia ili ibainike ni nani aliyeweka bango hilo.