Benki ya Dunia yatetea mpango wa Nyota unaokosolewa na vinara
BENKI ya Dunia imetetea mpango wa National Youth Opportunities Towards Advancement (Nyota), ambao umekosolewa na viongozi wa upinzani.
Mkurugenzi wa Benki ya Dunia nchini Kenya Qumiao Fan, alisema taasisi hiyo ya kimataifa ya kifedha iliunga mkono mpango huo kwa sababu umedhihirisha kuwa bunifu, shirikishi na wenye uwazi katika kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana nchini.
Kwa mujibu wa Bw Fan, ukosefu wa ajira bado ni mojawapo ya changamoto kubwa zinazolemaza maendeleo Kenya.
Akizungumza jana wakati wa uzinduzi wa mpango huo mjini Malindi, Kaunti ya Kilifi, alieleza kuwa mpango huo unaendana na malengo ya maendeleo ya Benki ya Dunia.
Hafla hiyo iliongozwa na Rais William Ruto.
“Mipango yetu yote imelenga kikamilifu kusaidia Kenya kuunda ajira bora na jumuishi zaidi. Kuanzia kuunga mkono mageuzi ya sera ili kurahisisha kufanya biashara, hadi kuwekeza katika nishati, barabara, teknolojia na sekta mahsusi kama kilimo, lengo kuu ni kusaidia kuundwa kwa ajira zaidi na tutaendelea kufanya hivyo,” alisema.
Licha ya kukosolewa na baadhi ya wanasiasa, Bw Fan alisisitiza kuwa kuwa shirika hilo litaendelea kusaidia serikali katika utekelezaji wake. Aliongeza kuwa mafanikio ya mpango huo yatapimwa mwishoni.
“Mwishowe, mafanikio ya Nyota yatapimwa kwa kuangalia ni kwa kiwango gani walionufaika watakuwa na uwezo wa kujiajiri na ni wangapi wataweza kuanzisha biashara, si kwa kujiajiri tu bali pia kuajiri wengine. Pia yatapimwa kwa idadi ya ajira zitakazoundwa,” alisema.
Viongozi wa upinzani waliokosoa vikali mpango huo ni pamoja na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na mwenzake wa United Green Movement (UGM), David Maraga.
Mapema Januari, Bw Musyoka alifananisha mpango huo na hongo kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Makamu wa rais wa zamani alihoji ni uwekezaji gani wa kibiashara unaoweza kufanywa kwa takribani Sh22,000 wanazopewa vijana.