Familia ya Boniface Kariuki yasubiri pumzi zake za mwisho
FAMILIA ya Boniface Kariuki, mchuuzi ambaye alipigwa risasi wakati wa maandamano sasa inasubiri tu mpigo wa moyo ukome, ili ithibitishwe amefariki akiwa katika Hospitali ya Kenyatta, Nairobi.
Kariuki, 22 alipigwa risasi kichwani karibu na jumba la Imenti wakati wa maandamano ya kusaka haki kutokana na mauaji ya bloga na mwalimu Albert Ojwang’ mnamo Juni 17.
Madaktari katika Hospitali ya Kenyatta walibaini kuwa ubongo wa Bw Kariuki umekufa na sasa kinachosubiriwa tu ni akate roho.

“Kile tunachosubiri na mpigo wa moyo ukome japo bado anapambana akiwa amewekewa mashine ya kuyaokoa maisha kwenye kitengo cha wagonjwa mahututi,” akasema Msemaji wa familia Emily Wanjira.
“Sheria za Kenya haziruhusu mashine zizimwe, kile tunachoweza kufanya sasa ni kusubiri tu hatima yake. Bili ya hospitali ni karibu Sh3 milioni na sasa tunatoa wito kwa wahisani waingilie watusaidie, akili ya mtu ikibainika imekufa, sasa hapo hakuna matumaini,” akaongeza Bi Wanjiru akiwa amejaa masikitiko.
Ubongo wa mtu ukifa, basi hiyo ina maana kuwa shughuli zote za mwili zimelemazwa na ni kama tu anayerejelewa ashakumbatia mauti.
Bi Wanjira alisema kuwa mnamo Alhamisi wiki jana, waliambiwa kuwa bado kulikuwa na kipande cha risasi ambacho kilikuwa kimekwama kwenye ubongo wa Bw Kariuki.
Bw Kariuki alikuwa akiuza barakao kabla ya kujipata kwenye tafrani kati ya waandamanaji na polisi ambapo alipigwa risasi.