Habari za Kitaifa

Gachagua asema ni mwanafunzi mwema wa Ruto kuhusu ‘hisa’

Na JUSTUS OCHIENG October 9th, 2024 Kusoma ni dakika: 1

NAIBU Rais Rigathi Gachagua ameanzisha mashambulizi makali ya moja kwa moja dhidi ya Rais William Ruto, akisema serikali imejaa ufisadi na mauaji ya kiholela ambayo waliahidi kukomesha walipokuwa wakifanya kampeni.

Katika utetezi wake dhidi ya hoja ya kumtimua mamlakani, inayoonyesha kuwa uhusiano wake na Rais Ruto umeharibika kiasi cha kutorekebika, Bw Gachagua alisema hawezi kukubali ukatili dhidi ya raia.

Bw Gachagua alitaja mashtaka 11 dhidi yake kama ya kipuuzi na kuwataka wabunge wazingatie sakata za ufisadi ambazo alisema zimejaa serikalini.

Katika mkutano na wanahabari katika makao yake ya Karen jijini Nairobi kabla ya kufika katika Bunge la Kitaifa kujitetea jana, Bw Gachagua aliwashambulia Maspika wa Mabunge mawili – Moses Wetang’ula (Bunge la Kitaifa) na Amason Kingi (Seneti) ambao alilaumu kwa kuwa sehemu ya mpango wa umiliki wa hisa za serikali.

“Wananishtumu kwa kuzua mgawanyiko na mkabila ninapozungumza kuhusu hisa ilhali ninaendeleza tu yaliyomo katika mkataba wao wa kabla ya uchaguzi waliotia saini na rais ambao ulikuwa umefichwa,” Bw Gachagua alidai.

Aliwashtumu Bw Wetang’ula na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi kwa kupatia kipaumbele masuala ya eneo lao la Magharibi, huku akimlaumu Bw Kingi kwa kujali maslahi yake mwenyewe ili awe spika wa Seneti badala ya kutetea maslahi ya eneo la Pwani anakotoka.

Pia, Bw Gachagua hakuwa na maneno mazuri kwa kinara wa upinzani Raila Odinga, ambaye alisema pia ameingia katika mpango wa hisa za serikali.

Alikuwa akirejelea kuundwa kwa Serikali Jumuishi ambayo viongozi wa zamani wa ODM waliteuliwa mawaziri.

Wanajumuisha waliokuwa naibu viongozi wa chama cha ODM Hassan Joho na Wycliffe Oparanya, aliyekuwa mwenyekiti wa kitaifa John Mbadi, aliyekuwa Mkurugenzi wa Masuala ya Kisiasa Opiyo Wandayi na aliyekuwa mwanachama wa bodi ya uchaguzi Beatrice Askul.
Naibu Rais anasisitiza kuwa alijifunza kutoka kwa bosi wake – Rais Ruto.