Habari za Kitaifa

Hali ya ufisadi Kenya yaingia hali ya kutia wasiwasi – Ripoti

Na STEVE OTIENO February 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HALI ya ufisadi nchini Kenya inaingia katika awamu ya kutia wasiwasi, huku takwimu mpya za kimataifa zikionyesha kuwa ufisadi hauendelei kuvuma tu bali umejikita zaidi katika mifumo ya utawala.

Ripoti ya hali ya Ufisadi ya mwaka wa 2025 inaonyesha kuwa nchi imekwama katika mzunguko wa mageuzi yasiyozaa matunda, ambapo taasisi za uwajibikaji bado ni dhaifu na imani ya umma inaendelea kudorora.

Ripoti hiyo inayochapishwa kila mwaka na Shirika la Transparency International (TI), hupima viwango vya ufisadi katika sekta ya umma kwa alama kati ya 0 na 100; sufuri ikiwa ni ufisadi uliokithiri na 100 ikiwa ni utawala safi usio na doa la rushwa.

Hukusanya tathmini za wataalamu na tafiti za wafanyabiashara kutoka taasisi huru, kisha kutoa wastani wa alama za kila nchi.

Katika toleo la 2025, Kenya ilipata alama 30 kati ya 100, ikishuka kutoka 32 mwaka wa 2024 na 31 mwaka wa 2023.

Kwa zaidi ya miaka 13, alama za Kenya zimekuwa zikizunguka kati ya 25 na 33, hali inayoonyesha ukosefu wa maendeleo ya maana licha ya kampeni na mageuzi ya mara kwa mara dhidi ya ufisadi.

Transparency International–Kenya (TI-Kenya) ilisema kushuka huko kunaashiria matatizo ya kimfumo badala ya kashfa za hapa na pale.

Mkurugenzi Mtendaji wa TI-Kenya, Sheila Masinde, alisema udhaifu huo umejikita katika mifumo ya ununuzi wa umma, upangaji wa bajeti, utoaji leseni na michakato ya udhibiti.

“Alama ya hivi karibuni inaonyesha kuwa ufisadi hauko tena katika matukio ya kipekee; umebadilika na kuwa mfumo sugu uliopenya katika ngazi zote za jamii na serikali, ukidhoofisha demokrasia, utawala wa sheria, uwazi na uwajibikaji,” alisema.

TI-Kenya ilitaja kutokuwajibishwa kama kichocheo kikuu. Kesi nyingi kubwa haziishii katika hukumu, nyingine hufutwa au kusuasua.

Hali hii imeimarisha mtazamo kwamba ushawishi wa kisiasa unaweza kuzidi mkono wa sheria.

Ingawa Katiba ina vifungu vya uongozi na uadilifu vinavyolenga kuwazuia wanaohusika na ufisadi kushika ofisi za umma, utekelezaji wake umekuwa dhaifu.

“Ili kukomesha ufisadi, sheria za kupambana na ufisadi, hasa vifungu vya uongozi na uadilifu, lazima zitekelezwe kikamilifu,” alisisitiza Bi Masinde.

Kikanda, Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ilipata wastani wa alama 32, ikiwa eneo lenye utendaji duni zaidi.

Rwanda ilipata alama 58 na Tanzania 40, zikifanya vizuri kuliko Kenya, huku Uganda (25) na Burundi (17) zikifanya vibaya zaidi Afrika Mashariki.

Kimataifa, Denmark iliongoza kwa alama 89, ikifuatiwa na Finland (88) na Singapore (84). Sudan Kusini na Somalia zilishika mkia kwa alama tisa.

Kwa Kenya, athari ni za kisiasa na kiuchumi. Ufisadi hupunguza fedha za huduma muhimu kama afya, elimu na miundombinu, huongeza gharama za miradi na kudhoofisha imani ya wawekezaji.

TI inapendekeza kuimarishwa kwa uhuru wa taasisi za haki, kulindwa kwa wanaofichua ufisadi kuongeza uwazi wa mifumo ya kidijitali kama ununuzi mtandaoni, na kudhibiti kwa ukali ufadhili wa kampeni za kisiasa.