Hii ndiyo serikali yetu ya kushibia, Raila aambia wafuasi Luo Nyanza
KINARA wa ODM Raila Odinga Alhamisi aliitaka ngome yake ya Nyanza iunge mkono serikali ya Rais William Ruto kwa dhati, akisema ndiyo pekee ambayo itastawisha eneo hilo kupitia miradi ya maendeleo.
Bw Odinga, aliwaambia wakazi wa Nyanza kwamba hakuna serikali nyingine ambayo itawafaa kuliko hii ya sasa, huku akipigia debe ushirikiano wake na Rais Ruto ndani ya Serikali Jumuishi.
“Tunataka kuimarisha maisha ya watu wetu sasa na hatuwezi kusubiri zaidi. Hatutaki kusubiri serikali nyingine na tunataka serikali hii ihudumie watu wetu,” akasema Bw Odinga akihutubia mkutano mkubwa wa kisiasa katika uwanja wa Kirembe, viungani mwa jiji la Kisumu.
“Kama si sasa ni sasa hivi na hii ndiyo maana niliingia kwenye mkataba na Rais Ruto kupitia chama chake cha UDA,” akaongeza huku akishangiliwa na umati.
Bw Odinga aliwataka watu kutoka eneo la Nyanza wamwaamini kwa sababu anajua mwelekeo ambao aliuchukua kwa kuridhiana na Rais ndipo wakaamua kufanya kazi pamoja.
“Mimi najua mahali tumetoka, mahali tupo na mahali tunaenda. Mko tayari?” akauliza umati ambao ulijibu ‘ndio’.
Waziri huyo mkuu wa zamani alisema utawala wa sasa ndio utafaa eneo hilo kupitia miradi ya maendeleo na hakuna sababu zozote za kuupiga vita.
Baadhi ya miradi aliyoitaja ni ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Naivasha-Kisumu-Malaba na ujenzi wa kituo kikuu cha kisasa cha viwanda katika eneo la Miwani, eneobunge la Muhoroni.
Pia aliunga mkono mradi wa ujenzi wa nyumba za bei nafuu akisema kuwa ni muhimu pamoja na maisha bora, elimu, chakula na afya.
“Lazima tuhakikishe kuwa sekta ambazo ni msingi wa uchumi wa eneo hili kama kilimo cha pamba, njugu na sekta ya uvuvi, zote zinafufuliwa,” akasema.
Kauli ya Bw Odinga inaonekana kuzima kabisa hatihati ambayo imekwepo kuhusu ushirikiano wake na serikali.
Suala hilo limekuwa likiwagawanya baadhi ya viongozi wa eneo hilo, mrengo moja ukiunga serikali na mwingine ukipinga ushirikiano kati ya ODM na UDA.
Akionekana kutiwa nguvu na kauli ya Raila, Rais Ruto alisema kuwa kwa sasa jukumu lake ni kuchapa kazi bila kupumzika.
“Nimekuja na Baba (Raila) hapa kwa sababu ya maendeleo na hayo ndiyo matarajio yenu kwetu. Mliniambia niunde Serikali Jumuishi kuunganisha nchi na niliwasikia, hii ndiyo inapeleka taifa letu mbele,” akasema Rais.
Pia alionekana kumlenga aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na vinara wengine wa upinzani ambao alisema wameanza kampeni za mapema za 2027 badala ya kumpa fursa ya kuchapa kazi.
“Kuna watu ambao wanataka tuchape siasa badala ya kufanya kazi. Nimewaambia waniache na Raila tufanye kazi kwanza.Ni watu ambao wamejawa na chuki, ukabila na wanaotaka kuharibu nchi yetu wala hatuna nafasi yao nchini,” akasema.
Rais alihakikishia hadhira yake kuwa ataendelea kuchapa kazi bila siasa huku akisema ushirikiano wake na Raila ndio utasababisha aafikie malengo yake mengi kwa Wakenya.
Rais aliweka jiwe la msingi katika ujenzi wa nyumba za bei nafuu Kirembe na pia kuwakabidhiufunguo wamiliki wapya wa nyumba zilizojengwa na serikali katika mtaa wa Makasembo.
Mtaa huo ulipewa jina la seneta wa kwanza wa Wilaya ya Nyanza ya Kati enzi za uhuru Dickson Oruko Makasembo.
Viongozi hao wawili wakuu waliandamana na Waziri wa fedha John Mbadi, Opiyo Wandayi (Kawi) Gavana wa Kisumu Profesa Anyang’ Nyong’o, Seneta wa Kisumu Tom Ojienda na Mbunge wa Kisumu ya Kati Dkt Joshua Odongo. Katibu katika Wizara ya Usalama wa Ndani Dkt Raymond Omollo pamoja na Naibu Gavana wa Kisumu Dkt Mathew Owili pia walikwepo.
Hii ilikuwa mara ya kwanza mwaka huu Rais na Bw Odinga kuandamana pamoja kwenye ziara ya Nyanza kwa kuwa kiongozi wa nchi amekuwa akitembelea eneo hilo akiwa ameandamana na viongozi wengine bila waziri huyo mkuu wa zamani.
Mnamo Disemba wawili hao walikuwa pamoja wakati wa Tamasha ya Piny Luo ambayo ilifanyika katika Kaunti ya Siaya.
Rais ataongoza maadhimisho ya 61 ya Madaraka katika uga wa Raila Odinga, Homa Bay mnamo Jumapili.