Hisia mseto zaibuka kuhusu Iftar ya pamoja Mapembeni
DAKIKA chache kabla ya jua kutua, eneo maarufu la Mapembeni katika barabara ya Moi Avenue mjini Mombasa hubadilika kutoka kuwa kivutio cha watalii wanaokusanyika kupiga picha, hadi kuwa eneo la futari ya pamoja.
Barabara hiyo hufungwa kwa muda wa saa chache, magari yakilazimika kutumia njia mbadala.
Baadaye zulia hutandikwa kwenye barabara hiyo, tende, maji na maankuli mengine kuwekwa tayari kwa Mwadhini.
Harufu nzuri ya vyakula na vitafunwa vya kila aina kama bhajia, sambusa, viazi karai, kaimati, na kahawa ‘thungu’ huvutia waliofunga na wasiofunga katika eneo la Mapembeni kujumuika na waumini wa Kiislamu kwenye Iftar ambayo huandaliwa kila ijumaa tangu msimu wa Ramadhani ulipoanza.
Vijana wa shirika la Swahilipot Hub Foundation ambao wamejitolea kugawa futari hiyo, hawasazi yeyote – mkubwa na mdogo, walioketi kwenye mazulia yaliyotandikwa kwenye sehemu hiyo.
Polepole, watu huanza kukusanyika hasa waliovalia kanzu.
Wafanyakazi kutoka maofisini humiminika Mapembeni baada ya siku ndefu, waendesha bodaboda huegesha pikipiki zao kando ya barabara, madereva wa tuktuk husimama pembeni, huku wazee wakitembea taratibu wakiwa na tasbihi mikononi mwao wakielekea Mapembeni kufungua.
Hata watoto wa kurandaranda mitaani hupata nafasi ya kula na matajiri kutokana na baraka za Ramadhani.
Ndani ya dakika chache, mamia ya watu huwa wameketi kwenye mikeka wakisubiri suala ya Maghrib itakayowaashiria wakati wa kufungua saumu.
Kwa wakazi wengi wa Mombasa, futari ya pamoja ambayo ilianzishwa wiki mbili zilizopita katika eneo la Mapembeni, itakuwa desturi muhimu ya Ramadhani mahali ambapo watu wote huketi pamoja na kufungua saumu baada ya siku ndefu ya kufunga.
“Tumeungana na jamii, watu binafsi na kampuni mbalimbali kuonyesha umuhimu wa dini na upendo wetu. Huu ndio uzuri wa Ramadhani, kushirikiana na kuhakikisha kila mtu anapata kitu cha kula,” alisema Bi Rukia Janwala, mkurugenzi wa shirika la Swahilipot Hub Foundation.
Alisema Iftar ya umati pia imeweza kushirikisha jamii zote za Mombasa.
Bi Janwala alisema mradi huo huandaliwa na wahisani wanaojitolea hasa makundi ya vijana.
Baadhi hukusanya michango kutoka kwa wahisani huku wengine wakipanga chakula na kuwaelekeza watu maeneo ya kuketi.
“Watu huchangia chochote wanachoweza tende au hata pesa. Kazi yetu ni kuhakikisha hakuna anayekosa kitu cha kufungua nacho,” alisema Bw Mahmoud Noor mwanzilishi wa shirika la Swahilipot Hub Foundation.
Alisema alianzisha mpango huo wa futari ya pamoja katika barabara hiyo ili kujumuika na jamii zote za Mombasa katika eneo hilo ambalo ni kituo cha utalii.
“Lengo kuu ni kuwaleta watu pamoja. Pia tunawalisha wale wasiokuwa wamefunga na kuwasaidia wasiokuwa na uwezo kupata mlo,” alisema.
Hata hivyo, umaarufu unaozidi kuongezeka wa mkusanyiko huo pia umevutia ukosoaji kutoka baadhi ya watu hasa madereva ambao walisema shughuli hiyo ya kila ijumaa husababisha msongamano wa magari katikati mwa mji huo hasa wale wanaoelekea bandarini.
“Si haki kufunga barabara kwa ajili ya kufungua saumu. Si wangekwua wanaenda katika bustani ya Mama Ngina kufungua? Mombasa ni jiji lenye shughuli nyingi, hasa katika barabara inayoelekea bandarini,” alisema Bw Morris Kioko, ambaye ni dereva.
Lakini kwa wakazi wengi, mkusanyiko huo unaonyesha roho halisi ya Ramadhani ukarimu, umoja, upendo na mshikamano wa jamii.
“Huenda humjui mtu aliyeketi karibu nawe lakini mnakula pamoja. Mnapofungua saumu pamoja, mnajihisi kuwa ndugu. Hiyo ndiyo maana ya Ramadhani,” alisema Bw Noor.
Gavana wa Mombasa, Abdulswamad Nassir, aliwashtumu wale ambao wanakosoa futari hiyo ya pamoja akisema inakuza upendo na kuishi kwa amani.
“Mpango huu unaleta umoja, na hiyo ndiyo roho ya Ramadhani. Waislamu na wasiokuwa Waislamu hukusanyika pamoja kufungua saumu. Pia inaonyesha kuwa kaunti yetu iko salama na ina amani,” alisema.