Habari za Kitaifa

Hofu kuhusu amri ya kutimua jamii ya Ethiopia Mandera

Na MANASE OTSIALO February 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HOFU imezuka katika Kaunti ya Mandera kutokana na amri ya wenyeji na wanasiasa wa eneo hilo kuwa jamii ya Wolaita warejee kwao Ethiopia na wamepigwa marufuku katika gatuzi hilo.

Watu kutoka jamii ya Wolaita waliingia Mandera zaidi ya miaka 30 iliyopita wakitoroka vita vya ukoo, mateso, njaa na changamoto nyingine kwao Ethiopia.

Kwa kipindi hiki wameishi Mandera bila tatizo lolote tena kwa amani lakini sasa koo za eneo hilo zimesema hawatakiwi kuendelea kuishi Mandera na kuamrisha wafutwe.

“Hawa ni watu ambao hawana stakabadhi za kuwatambua na wanaleta matatizo mengi Mandera. Uwepo wao umesababisha kuongezeka kwa uhalifu katika miji yetu na tunataka waende,” akasema Mbunge wa Mandera Mashariki Hussein Weyten.

Mbunge huyo alidai kuwa wameafikiana na asasi za kiusalama ili Wolaita warejeshwe kwao Ethiopia.

“Wamevuruga tamaduni yetu hapa,” akaongeza mbunge huyo.

Shinikizo za kuwataka Wolaita waondoke Mandera ziliibuliwa na viongozi wa kidini kuelekea mwisho wa 2025.

Wengi wa watu kutoka jamii hiyo wameajiriwa kama wafanyakazi wa nyumbani, wa shambani, wauzaji kwenye maduka na ni wafanyabiashara ndogondogo.

Mnamo Januari 19, 2026 wawakilishi wa jamii walitangaza amri kuwa jamii ya Wolaita wanatakiwa waondoke Mandera kufikia Februari 5.

Amri hiyo iliyothibitishwa na Mzee wa Ukoo Osman Rakiso pia iliwaonya wakazi dhidi ya kuwa wenyeji wao.

Diwani wa Mandera Mjini Feisal Abdinoor alisema juhudi zake za kupinga amri hiyo zilizidiwa na shinikizo za kijamii.

“Siungi mkono wazo hilo lakini kwa sababu wenyeji walinilemea sikuwa na jingine ila kukubali. Wolaita wataenda lakini tutahisi athari za kuondoka kwao,” akasema Bw Abdinoor.

“Sijaona sababu zenye mashiko za kuwafurusha na kama uhalifu umeongezeka basi sheria ichukue mkondo wake. Pia tungewakubali na kusaka njia ya kuwatambua,” akaongeza.

Baada ya amri kutolewa, magari yaliyowekewa vipaaza sauti yalizunguka mji wa Mandera na kutangaza kuondoka Wolaita wataondoka kwenye kaunti hiyo.

Hata hivyo, baadhi ya watu wa jamii hiyo wameshangaa kwa nini wanafurushwa huku wakikanusha wamekuwa wakishiriki uhalifu na kutatiza amani.

“Nimeishi Mandera kwa zaidi ya miaka 30 na nimeshtuka kuwa watu ambao nimetangamana nao muda huu wote ndio wamenigeuka. Wamenifukuza kutoka mjini,” akasema Admasu Oyda Bade akijiandaa kuvuka Mto Dawa ambao ni mpaka wa Kenya-Ethiopia.

Gavana wa Mandera Mohamed Adan Khalif amejitokeza hadharani kuunga kufurushwa kwa jamii hiyo ya Ethiopia akisema wanatumia rasilimali za kaunti na pia kushiriki uhalifu.

Wolaita wamelalamika kuwa sasa wanahangaishwa na maafisa wa usalama baada ya amri ya kuwatimua kutolewa.

Kamishina wa Kaunti ya Mandera James Chacha hata hivyo alikana kufahamu mpango wa kutimua jamii ambao makataa yake yashapita.

“Sifahamu mpango huo wala hata sijui kuna jamii inaitwa Wolaita inaishi Mandera. Lazima niulize kisha nikwaambie baadaye,” akasema Bw Chacha.

Kamishina wa Ukanda wa Kaskazini Mashariki John Otieno alikanusha kuwa anafahamu chochote kuhusu amri hiyo.

“Sifahamu kuhusu mpango wa kutimua jamii na iwapo upo basi haujafika afisi yangu,” akasema Bw Otieno.