Ikulu yageuka tumbo lisiloshiba ikimeza Sh17 bilioni kufikia katikati ya mwaka
BAJETI ya Ikulu ya mwaka wa kifedha 2025/26 imepanda maradufu kufikia Sh16.998 bilioni kufuatia kutengewa pesa zaidi kati kati ya mwaka ambayo ni matumizi bila idhini ya Bunge.
Makadirio ya bajeti ya ziada kwa mwaka wa kifedha wa sasa, yaliyowasilishwa mbele ya Bunge yanaonyesha kuwa, bajeti ya Ikulu iliongezeka kwa Sh8.42 bilioni.
Kupatiwa pesa zaidi kati kati ya mwaka kulifanya matumizi ya kila mwaka ya Ikulu kuzidi ya ofisi zinazofanana katika nchi zilizoendelea kama Amerika (Sh10 bilioni), Ujerumani (Sh7 bilioni), Ureno (Sh2.6 bilioni) na karibu kufikia ile ya Ufaransa (Sh17.5 bilioni).
Karibu na nyumbani, matumizi ya Ikulu ya Kenya yalikuwa ya juu kuliko Nigeria (Sh3.1 bilioni), Afrika Kusini (Sh7.8 bilioni), Algeria (Sh8.9 bilioni) na Tanzania (Sh1.7 bilioni).
Sh16.998 bilioni ni kiasi kikubwa zaidi kilichotumika na Ikulu tangu 2013.
Haya yanajiri huku Mdhibiti wa Bajeti (CoB) Dkt Margaret Nyakang’o akitoa onyo kuhusu uwezekano wa Ikulu kutumia bajeti yake yote mapema katikati ya mwaka wa kifedha.
Stakabadhi zilizowasilishwa Bungeni na Waziri wa Fedha John Mbadi zikitaka idhini ya wabunge kwa matumizi ya ziada zinaonyesha kuwa, Ikulu kwanza iliomba Sh2 bilioni “kwa matumizi mengine ya uendeshaji,” ambayo si dharura, Septemba 8 2025.
“Kufuatia idhini ya bajeti ya mwaka wa kifedha 2025/26, Wizara ya Fedha imetoa fedha za ziada kwa Wizara, Idara na Mashirika kulingana na katiba,” alisema Waziri Mbadi katika stakabadhi zilizowasilishwa Bungeni.
Maombi haya ya fedha za ziada yameelezwa kuwa ya kuimarisha operesheni na ukarabati katika Ikulu.
Mnamo Juni 2025, Bunge lilitengea Ikulu Sh8.6 bilioni, ikiwa ni Sh7.7 bilioni kwa matumizi ya kawaida na Sh894.91 milioni kwa maendeleo.
Hata hivyo, bajeti ilipanda hadi Sh16.998 bilioni kufikia Februari, huku Sh16.1 bilioni zikiwa kwa matumizi ya kawaida na maendeleo yakiwa Sh894.91 milioni tu.
Stakabadhi zinaonyesha iliomba Sh4.5 bilioni chini ya Kifungu cha 223 Septemba 2025, miezi mitatu tu baada ya kuanza kwa mwaka wa kifedha, baada ya bajeti ya awali kutumika.
Wizara ya Fedha baadaye ilikubali na kutoa Sh4.4 bilioni tarehe mbalimbali.
Kifungu cha 223 cha katiba kinaruhusu serikali ya kitaifa kupata fedha za ziada pale ambapo bajeti iliyotengwa na Bunge inakosa kutosha au kukitokea dharura isiyoweza kuepukika kama ukame, mafuriko au janga lisilotarajiwa.
Makadirio ya bajeti ya Ikulu kwa mwaka wa kifedha 2025/26, yaliyopitishwa na Bunge Juni 2025, yalikuwa Sh8.58 bilioni na kisha yakapanda hadi Sh16.998 bilioni, ikiwa ni ongezeko la Sh3 bilioni zaidi mwaka wa kifedha 2024/25.
Wataalamu wa fedha katika Ofisi ya Bajeti ya Bunge (PBO) wanasema ombi hili ni ukiukaji wa katiba na udhaifu wa nidhamu ya kifedha.
Dkt Nyakang’o alionya kuwa ingawa Ikulu ilionyesha utendaji bora, ikiwa na kiwango cha matumizi cha asilimia 55, juu zaidi ya wastani wa robo ya kwanza wa asilimia 25, bado ipo hatarini kufyonza bajeti yake mapema kabla ya mwisho wa mwaka wa kifedha, jambo linalohujumu uhalali wa bajeti.
Huduma za Ikulu ni pamoja na kuratibu kazi za Ikulu na usimamizi wa mafao ya kifedha kwa marais na makamu wa rais waliostaafu.
Katika robo ya kwanza ya mwaka huu wa kifedha, kuratibu kazi za Ikulu kuligharimu Sh4.7 bilioni, ikiwa ni Sh4.45 bilioni kwa matumizi ya kawaida na Sh235.10 milioni kwa maendeleo.
Kwa mafao ya kifedha ya marais na makamu wa rais waliostaafu, Sh452.6 milioni zilitengwa, huku Sh50.59 milioni zikiwa zimetumika tayari.