Iran yashtumu Kenya kwa kutoadhibu waliohusika na kashfa ya chai
IRAN imeeleza wasiwasi mpya kuhusu kile inachotaja kama kusuasua kwa Kenya kuchukua hatua dhidi ya maafisa na wafanyabiashara wanaohusishwa na kashfa ya usafirishaji wa chai mwaka 2023 ya thamani ya Sh2.6 bilioni.
Mgogoro uliotokana na shehena hiyo tata uliifanya Tehran kufunga ghafla mojawapo ya masoko muhimu ya Kenya, hali iliyowaacha maelfu ya wakulima wadogo wa chai bila wanunuzi.
Balozi wa Iran nchini Kenya Ali Gholampour, alisema kuwa Tehran tayari imewashtaki na kuwaadhibu raia wake waliotajwa katika sakata hiyo, huku akiihimiza Nairobi kuharakisha mchakato wa kuwajibisha waliohusika mazungumzo ya kumaliza mvutano wa kibiashara yakiendelea.
Katika mahojiano, balozi huyo alisisitiza kuwa uwajibikaji ni muhimu na kwamba Iran imechukua hatua madhubuti za kisheria.
“Nchini Iran, waliohusika katika mpango huo wa ulaghai tayari wamefikishwa mahakamani na kuadhibiwa, wakiwemo maafisa wakuu na kinara wa sakata hiyo, waliopokea vifungo virefu na kuamriwa kurejesha mabilioni ya pesa kwa Serikali,” alisema Gholampour, akisisitiza hatua kali zilizochukuliwa.
Aliongeza kuwa ushirikiano wa Kenya sasa ni muhimu ili kurejesha imani na kufungua tena biashara ya chai.
Balozi huyo alisema nchi hizi mbili zinakusudia kuongeza biashara ya pande mbili mara tano hadi kufikia Sh129 bilioni kwa mwaka ndani ya muongo mmoja ujao.
Kashfa hiyo inahusisha kampuni ya Irani ya Debsh na ya Kenya Cup of Joe, katika mzozo ulioanza mwaka 2023 na kusababisha Iran kupiga marufuku uagizaji wa chai ya Kenya.