Joto lapanda siku mbili kabla maandamano ya kuadhimisha Juni 25
MIHEMKO tayari imeanza kupanda kuelekea maandamano ya Jumatano ambayo yamepangwa kuandaliwa na Gen Z kuadhimisha mwaka moja tangu wavamie majengo ya bunge na kuwaombea wenzao waliopoteza maisha.
Maandamano hayo yamezua tubo joto miongoni mwa viongozi ambao wanaegemea mrengo wa serikali huku wale wa upinzani nao wakionekana kuwatia vijana mori na kuahidi kuungana nao.
Huku familia za Gen Z hao zikisaka haki na kutangaza kuwa zitashiriki maandamano hayo, wanasiasa wa serikali nao wameeleza hofu kuwa maasi hayo huenda yakaishia uharibifu wa mali na maafa na inastahili kukomeshwa kabisa.
Mwaka jana, vijana walikuwa barabarani kupinga Mswada wa Fedha 2024 ambao ulisheheni nyongeza ya ushuru na jitihada zao zilifanya Rais Ruto kuondoa mswada huo.
Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetangúla, Kiongozi wa Wengi Kimani Ichung’wah mwenzake wa Seneti Aaron Cheruiyot na Msaidizi wa Rais William Ruto, Bw Farouk Kibet wamedai kuwa kuna viongozi wa upinzani wanaoshiriki uchochezi na kufadhili maandamano hayo na wakata idara ya usalama ikae ange.
“Mwaka jana waliwaleta vijana barabarani kwa lengo la kuangusha utawala wa Rais William Ruto ili kumwondoa ikuluni. Wanawachochea vijana na kupanga ghasia mnamo Jumatano lakini mara hii hatutaruhusu hilo,” akasema Bw Ichung’wah.
Viongozi hao walikuwa wakizungumza katika eneobunge la Navakholo ambapo walidai aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ndiye anadhamini maandamano ya Gen Z na hata alifanya hivyo alipokuwa serikalini.
Bw Wetangúla alisema kuwa maandamano hayo yanawaathiri wafanyabiashara wadogo wadogo ambao wanalenga kuyaongeza mapato yao lakini hupata pigo biashara zao zikiporwa.
“Vijana wetu wanatumiwa vibaya na upinzani kusababisha taharuki na kuharibu mali. Wale ambao wanaitisha maandamano pia lazima wawajibike iwapo kutakuwa na uporaji na uharibifu wa mali,” akasema Bw Wetangúla.
Spika huyo alitoa wito kwa polisi wawe ange na wachukue hatua kali dhidi ya wale ambao watavuruga amani, wataharibu mali akisema uhuru wa kusaka haki haufai kuwadhulumu wengine.
Bw Cheruiyot alitoa wito kwa Jaji Mkuu Martha Koome ahakikishe kuwa kesi ambazo wahuni huharibu mali na kushiriki uporaji wa mali zinaamuliwa haraka ili iwe funzo kwa wanaoshiriki uhalifu.
“Watu hawa wanatekeleza uhalifu kisha wanakimbia kujificha kortini. Tunataka Idara ya Mahakama iharakishe kesi ambapo washukiwa hushtakiwa.
“Mahakama hazifai kuwa maficho kwa uhalifu ila wawakabili washukiwa. Kwa nini inachukua muda kwa mahakama kuwaadhibu wale ambao walichoma nchi yetu na bado wanaruhusiwa kufanya maovu zaidi?” akauliza Seneta huyo wa Kericho.
Mbunge wa Mugirango Kusini Silvanus Osoro naye alitoa wito kwa polisi wawe macho ili kupambana na yeyote mwenye nia ya kusababisha maovu.
Bw Osoro alitoa wito kwa vijana wajiepushe na maandamano ya Jumatano na akaitaka mahakama ihakikishe kuwa wanaovunja sheria nao wanachukuliwa hatua kali.
“Wakisababisha ghasia, uchumi nao huathirika na wale ambao huumia zaidi ni watu maskini. Hata wale ambao huenda maandamano na kujeruhiwa au kuuawa ni wale ambao ni maskini,” akasema Bw Osoro.
Mitandaoni, vijana tayari wanashaajishana kupambania haki za wenzao huku maandamano ya Jumatano yakija wakati ambapo kwa Jumanne ya wiki juzi na wiki jana, kumekuwa na makabiliano kati ya vijana kwa upande mmoja kisha magenge, na polisi kwa upande mwingine jijini Nairobi.
Kumekuwa na maandamano ya kusaka haki kwa familia ya Mwalimu na Bloga Albert Ojwang’ ambaye alikufa mikononi mwa polisi wiki mbili zilizopita suala hilo likisababisha Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat ambaye alikuwa mlalamishi kujiondoa afisini kwa muda.
Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja mwishoni mwa wiki alikubali maandamano hayo ambayo kilele chake kitakuwa ibada ya maombi bustani ya Uhuru Park yaendelee, lakini akasema polisi watakuwa macho kutibua jaribio lolote la fujo na uporaji wa mali.
Viongozi wa upinzani wakiongozwa na Bw Gachagua, Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa wa DAP Kenya na Martha Karua wa PLP nao wamesema kuwa wapo nyuma ya Gen Z Jumatano na hata kutaja siku hiyo kama sikukuu ya taifa wakitaka watu wasiende kazi.