Habari za Kitaifa

JUMATANO NYEUSI: Sita wafariki polisi wakikabili waandamanaji wa Juni 25

Na WAANDISHI WETU June 26th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

WATU sita walifariki Jumatano, Juni 25, 2025 baada ya kupigwa risasi na polisi maelfu ya waandamanaji walipoingia barabarani kote nchini kukumbuka vijana waliouawa katika maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha 2024.

Wawili walifariki mjini Matuu, Kaunti ya Machakos, wawili wakafa Emali, Kaunti ya Makueni mwingine akafariki Molo, Kaunti ya Nakuru kutokana na majeraha ya risasi huku wa sita akiripotiwa kufariki katika Ol Kalou, Kaunti ya Nyandarua.

Msimamizi wa hospitali ya kaunti ndogo ya Matuu Bw Julius Makau alisema, hospitali hiyo ilipokea wagonjwa tisa waliokuwa wamejeruhiwa baada ya polisi kufyatua risasi kwa waandamanaji waliokuwa wakichoma matairi na kujaribu kuvamia Kituo cha Polisi cha Matuu.

“Watu sita walikuwa na majeraha ya risasi. Mwanaume aliyefariki alipigwa risasi tumboni. Mwingine ambaye hali yake ni mahututi baada ya kupigwa risasi kichwani alifariki alasiri. Wahasiriwa wengine watatu walipata majeraha madogo yaliyochangiwa na mambo mengine,” alisema Bw Makau.

Waliouawa Eldoret na Molo walikuwa wakiandamana kwa amani polisi walipowafyatulia risasi.

Maelfu ya vijana walimiminika barabarani katika miji tofauti nchini kuadhimisha mwaka mmoja tangu vifo vya waandamanaji waliouawa wakipinga serikali mwaka jana.

Maandamamo hayo yalifanyika katika miji zaidi ya 26 nchini.

Vijana walimiminika katikati ya jiji licha ya polisi kuweka vizuizi kudhibiti magari na walioingia jijini.

Maandamano yalichacha Kisii, Kiambu, Githurai, Kitengela, Mlolongo, Nyeri, Nakuru, Karatina,Mombasa, Nyahururu, Wote, Meru, Embu, Machakos, Matuu, Kakamega, Busia, Bungoma Kericho miongoni mwa miji mingine.

Shughuli zote zilisimama katikati ya miji na mitaa ambako wakazi waliandamana.

Lori la polisi lilichomwa Eldoret na maduka kadhaa yakavunjwa na kuporwa katika baadhi ya miji.

Jijini Nairobi, maandamano yalichacha, huku polisi wa kukabiliana na ghasia wakirusha vitoa machozi kuwatawanya waandamanaji.

Vijana walifika katikati ya jiji licha ya barabara nyingi kufungwa asubuhi na shughuli za usafiri kuvurugika. Biashara nyingi zilifungwa huku hofu ikitanda miongoni mwa wafanyabiashara.

Polisi waliimarisha ulinzi katika majengo ya serikali, hasa Bunge na Ikulu, huku vizuizi vya usalama vikiwekwa ili kuzuia umma kufika maeneo hayo muhimu.

Katika miji ya Nakuru na Mombasa, hali ilikuwa karibu sawa na ile ya Nairobi, ambapo vijana waliandamana wakiimba nyimbo za haki na kutaka serikali iwajibike kwa vifo vya waandamanaji mwaka jana.

Mjini Nakuru, waandamanaji walifunga barabara kuu huku wakielekea katikati ya mji wakipinga sera za serikali.

Katika jiji la Nairobi, ripoti zinaonyesha watu kadhaa waliopata majeraha ya risasi na walipokea huduma ya kwanza katika kambi za matibabu zilizowekwa katikati ya jiji.

Kambi moja karibu na msikiti wa Jamia ilikuwa na shughuli nyingi, ambapo wahudumu wa afya walijitahidi kuokoa maisha ya waandamanaji waliokuwa wamejeruhiwa.

Daktari Simon Kigondi, Rais wa Chama cha Madaktari Kenya (KMA), alisema walipokea wagonjwa waliopata majeraha mbalimbali, baadhi yao wakiwa na majeraha ya risasi, wengine wakiwa wamevunjika mikono au kujeruhiwa kichwani kutokana na mawe.

“Tumepokea majeruhi wa aina zote. Wapo waliopigwa mawe kichwani, wengine walichomwa na vitoa machozi na pia tuna waliopigwa risasi. Tunashauri waandamanaji waepuke kushika au kukaribia vitoa machozi,” alisema Dkt Kigondi.

Aliongeza kuwa, wagonjwa wanaopata huduma ya kwanza katika kambi hizo wanapelekwa hospitali ya Kenyatta kwa matibabu zaidi.

Afisa wa kike wa polisi alipigwa na kujeruhiwa vibaya na kundi la waandamanaji waliokuwa na hasira.

Waandamanaji walianza kuimba wakidai polisi ni wauaji, na kabla ya muda mfupi, waliwapura mawe maafisa hao ambao walikimbia kwa usalama wao.

Kwa bahati mbaya, afisa huyo wa kike aliteleza wakati wa kukimbia kuelekea barabara ya Muindi Mbingu kutoka Kenyatta Avenue na akaachwa nyuma na wenzake lakini waandamanaji waliingilia kati na kumuokoa na kumpeleka kwa matibabu katika kambi ya dharura.

Ingawa maandamano hayo yalianza kwa amani katika maeneo mengi, hali ilibadilika polisi walipoanza kutumia nguvu dhidi ya waandamanaji.

Milio ya risasi na milipuko ya vitoa machozi ilichana anga polisi wakikabili waandamanaji katikati ya jiji la Nairobi huku vijana wakikabiliana na polisi tangu saa tatu na nusu asubuhi serikali ikilenga kuzima maandamano.

Vijana walikuwa wakitawanywa na kisha kukusanyika kwa nguvu na kurejea barabarani kuendelea kuimba wakitaka haki kwa wenzao zaidi 60 waliouawa mwaka jana wakipinga Mswada wa Fedha 2024. Wakati mmoja, waandamanaji walifika katika kituo cha polisi cha Central, Nairobi lakini wakatawanywa kwa vitoa machozi.

Usalama uliimarishwa vikali katika jiji la Nairobi kuanzia asubuhi huku maafisa wa polisi wakifunga barabara kuu zinazoelekea katikati ya jiji.

Hata hivyo, vijana walifaulu kufika jijini na kuanza maandamano huku maduka yakifungwa na magari yakiwa machache mno.

Katika Kaunti ya Nyeri, maandamano yafanyika katika mji wa Nyeri na maeneo mengine ya kaunti hiyo.

Usafiri katika barabara kuu ya Nyeri-Karatina ulitatizika kabisa huku magari ya umma na binafsi yakikwama kutokana na maandamano hayo.

Milipuko ya vitoa machozi ilitikisa anga katika mji wa Embu na Meru jana huku polisi wakikabiliana na vijana waliokuwa wakiandamana wakishinikiza mabadiliko ya kisiasa na haki kwa waliopoteza maisha katika maandamano ya mwaka jana.

Biashara zote zilifungwa kwa haraka huku wafanyabiashara wakihofia uporaji, hali iliyosababisha shughuli katika mji mzima kukwama.