Habari za Kitaifa

Kaunti zinatumia wanafunzi kusajili kampuni hewa za kupora pesa, EACC yasema

Na RUSHDIE OUDIA June 27th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

TUME ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) imefichua mpango wa ambapo maafisa wa juu wa serikali za kaunti, wakiwemo magavana, wanadaiwa kuwahusisha wanafunzi walio kwenye mafunzo ya kazi kama njia ya kufuja mabilioni ya pesa za umma kupitia kampuni hewa.

Kulingana na EACC, maafisa wakuu wa kaunti wanashirikiana na wafanyakazi wa chini na wanafunzi kusajili kampuni bandia, kisha kutumia kampuni hizo kupokea fedha zinazotengwa kwa miradi ya maendeleo.

Katika hotuba iliyosomwa kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu Abdi Mohamud na Meneja wa Kanda ya Magharibi, Bw Eric Ngumbi, ilibainika kuwa wanafunzi hao kwa kujua au bila kujua wamekuwa kama kinga kwa maafisa wafisadi, huku wao wakiishia kuwa washukiwa wakuu katika kesi za ufisadi.

“Tunaona mwenendo mpya na wa kutia wasiwasi ambapo maafisa wakuu wa kaunti, wakiwemo mawaziri wa kaunti, wanazidi kuwatumia vijana kama njia ya kupora fedha za umma. Wanafunzi wanalazimishwa kusajili kampuni ambazo baadaye hupokea malipo yaliyokusudiwa kwa wasambazaji wa bidhaa na wakandarasi halali,” alisema Bw Mohamud.

Wanafunzi hao, wengi wao wakiwa hawajui uzito wa kisheria wa vitendo vyao, pia wanadaiwa kutumiwa kutoa pesa kwa niaba ya maafisa wafisadi.

Ripoti hiyo pia inasema kuwa makarani wa maafisa wakuu wanahusishwa na mpango huo.

“Maafisa wakuu wa kaunti, wakiwemo magavana, wanawalazimisha wanafunzi na wafanyakazi wa chini kuchukua mamilioni ya pesa kwa huduma m ambazo hazitolewi na kisha kuwapa wakubwa wao,” Bw Mohamud alieleza.

Alisisitiza kuwa pesa hizo zinapaswa kutumwa moja kwa moja kwa akaunti za watu wanaohitaji huduma hizo kwa matumizi halali si kupitishwa kwa mawakala wa wahusika wa ufisadi.

“Wafanyakazi wa ngazi za chini hawapaswi kukubali kutumiwa. Siku ya hukumu ikifika, kisingizio cha ‘niliamrishwa’ hakitasaidia. Sheria za kupambana na ufisadi hazitoi kinga kwa yeyote,” alionya.

Ufichuzi huu ulitolewa wakati wa uzinduzi rasmi wa warsha ya siku tatu ya kujenga uwezo wa uadilifu na kupambana na ufisadi kwa viongozi wa ngazi ya juu wa serikali ya kaunti ya Bungoma.

EACC inasema kuwa huu ni miongoni mwa mitindo ya ufisadi inayochunguzwa kwa sasa katika kaunti mbalimbali nchini.

Bw Mohamud alifafanua kuwa uporaji wa mali ya umma na maafisa wa serikali sio tu ukiukaji wa maadili bali ni usaliti kwa kiapo cha ofisi na zaidi, ni kusaliti wananchi wanaowaamini viongozi wao kulinda maslahi yao.

“Tusisahau kuwa ufisadi huota mizizi pale ambapo viongozi waliokula kiapo cha kuhudumia wananchi wanavunja uaminifu wa umma na kushiriki kuiba mali ya umma. Ufisadi huendelea pale ambapo uwajibikaji ni dhaifu na hali ya kutojali inaachwa uendelee. Kila shilingi inayopotea inamnyima mtoto elimu, mama matibabu na jamii maendeleo,” aliongeza.

Aidha, alitoa onyo kali kuhusu uwezekano wa kuongezeka kwa ufisadi kuelekea mwisho wa mwaka wa kifedha wa 2024/2025 utakaoisha Juni 30, 2025.

Tume hiyo imesema inafuatilia kwa karibu mipango ya kughushi malipo au kuhamisha fedha zilizotengewa wauzaji halali, hali ambayo mara nyingi husababisha madeni hewa au yasiyo halali.

“EACC iko macho na inawakumbusha maafisa wote wa uhasibu kuwa wana wajibu mkubwa wa kisheria kusimamia fedha za umma kwa uaminifu. Yeyote atakayepatikana kuhusika au kuidhinisha malipo yasiyo halali atawajibika binafsi,” alionya Bw Mohamud.